Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UN yasikitishwa na jaribio la kuuawa Waziri Mkuu wa Sudan

Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamdok katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa
Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamdok katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa
Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamdok katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

UN yasikitishwa na jaribio la kuuawa Waziri Mkuu wa Sudan

Amani na Usalama

Waziri Mkuu wa Sudan Abdalla Hamdok amenusurika jaribio la kuuawa lililotekelezwa hii leo jumatatu katika mji mkuu Khartoum

Baadaye Waziri Mkuu huyo kupitia katika mtandao wa Twitter ameeleza kuwa yuko “salama na katika hali nzuri.”

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stéphane Dujarric, akiwaarifu wanahabari katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York amesema, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ameshitushwa na kusikitishwa baada ya kusikia kuhusu shambulizi hilo na akaeleza kwamba yuko pamoja na Waziri Mkuu na watu wa Sudan.

Pia ujumbe wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa Afrika wa kulinda amani jimboni Darfur, UNAMID umetoa taarifa ya ukieleza masikitiko yake kuhusu jaribio hilo la mauaji.

Mwakilishi Maalum wa UNAMID, Jeremiah Mamabolo, amesema "sote tunashtushwa sana na kusikitishwa na tukio hili kubwa. Ni dhahiri kwamba mhusika (wahusika) wa kitendo hicho kibaya analenga kuvuruga kipindi cha mpito. Matarajio ya watu wa Sudan kuelekea katika amani, uhuru na haki lazima vishinde."

Bwana Hamdok aliteuliwa kuongoza serikali ya mpito mnamo mwezi Agosti baada ya kiongozi wa muda mrefu bwana Omar al-Bashir kuondolewa madarakani na majeshi kufuatia miezi kadhaa ya maandamano ya kuuupinga utawala wake.

Vyombo vya habari vimeripoti kuwa shambulio lilitokea baada ya bomu kupiga gari la Waziri Mkuu huyo lakini hakuna aliyejeruhiwa.

Vyombo hivyo vya habari vimenukuu mashuhuda wa tukio hilo wakisema kuwa shambulio hilo lilitokea karibu na kaskazini mashariki mwa mwanzo wa daraja la Kober, ambalo linaunganisha kaskazini ya Khartoum na mjini, eneo ambalo waziri mkuu anaishi.