Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mgonjwa wa mwisho wa Ebola DRC aruhusiwa kurejea nyumbani, 46 bado wanachunguzwa

Manusura wa Ebola akifanya kazi katika kituo cha kulea watoto katika eneo la Butembo mashariki mwa DRC (Agosti 2019)
UN Photo/Martine Perret
Manusura wa Ebola akifanya kazi katika kituo cha kulea watoto katika eneo la Butembo mashariki mwa DRC (Agosti 2019)

Mgonjwa wa mwisho wa Ebola DRC aruhusiwa kurejea nyumbani, 46 bado wanachunguzwa

Afya

Taarifa ya shirika la afya ulimwenguni WHO iliyotolewa jana mjini Brazzaville Congo na Goma Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, imesema kuwa habari njema ni kuwa mgonjwa wa mwisho wa Ebola nchini DRC ameruhiswa kurejea nyumbani baada ya kupatiwa matibabu katika kituo cha matibabu huko kaskazini mashariki mwa mji wa Beni.

Kukiwa hakuna kisa kingine chochote kipya kilichothibitika, tangu Machi pili, zimesalia siku 42 kuelekea kutangazwa kufikia mwisho wa mlipuko wa Ebola, wa pili kwa ukubwa duniani. Ni utaratibu uliopo kuwa ili kutangaza mwisho wa mlipuko wa ugonjwa ni lazima zipite siku 42 tangu mara ya mwisho mgonjwa wa mwisho alipopimwa na kukutwa bila maambukizi.

Ingawa mgonjwa wa mwisho wa Ebola ameruhusiwa kurejea nyumbani, WHO inasema inaendelea kuwafuatilia kwa ukaribu sana watu 46 ambao kwa namna moja au nyingine walikutana na mgonjwa huyo kabla ahajapatiwa matibabu.

Mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika Dkt Matshidiso Moeti amesema, “ninazipongeza juhudi za bila kuchoka ambazo zimefanywa kushughulikia mlipuko huu na ninahamasishwa na taarifa za kuwa mgonjwa wa mwisho wa Ebola ameondoka katika kituo cha tiba akiwa mwenye afya njema. Bado siyo mwisho wa Ebola katika DRC. Tunatakiwa kukaa chonjo katika wiki zijazo na kuendelea.”

Mlipuko wa hivi sasa ambao ulitangazwa mnamo tarehe mosi ya mwezi Agosti 2018, ni wa kumi katika nchi ya DRC na wa pili kwa ukubwa kidunia baada ya ule wa mwaka 2014 hadi 2016 huko Afrika Magharibi. Hadi kufikia tarehe mosi ya mwezi huu wa Machi, kulikuwa na visa 3444 vilivyothibitishwa na vilivyohisiwa kuwa ni ugonjwa huo, huku kukiwa na vifo 2264.

Bado juhudi za ufuatiliaji, upimaji na utoaji taarifa ikiwemo kushirikiana na mamlaka hadi ngazi ya jamii zinaendelea ili kufuatilia hali katika jamii.