Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

 Chonde chonde tushikamane kusaka suluhu ya wakimbizi wa ndani:Guterres

Mwanamke akiwa amesimama katika kambi ya wakimbizi wa ndani Maiduguri, jimbo la Borno, NIgeria.
OCHA
Mwanamke akiwa amesimama katika kambi ya wakimbizi wa ndani Maiduguri, jimbo la Borno, NIgeria.

 Chonde chonde tushikamane kusaka suluhu ya wakimbizi wa ndani:Guterres

Wahamiaji na Wakimbizi

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kushikamana katika kukabiliana na changamoto ya wakimbizi wa ndani wakati akifungua mkutano wa jopo jipya la ngazi ya juu kuhusu wakimbizi wa ndani mjini Geneva Uswis.

Akizungumzia uzinduzi wa jopo hilo hii leo mbele ya waandishi wa habari Rhéal LeBlanc, mkuu wa habari na uhusiano wa nje  amesema Jopo hilo ambalo liliundwa na Katibu Mkuu Oktoba 2019 linasimamiwa na Bi. Federica Mogherini aliyekuwa mwakilishi wa Muungano wa Ulaya kwa ajili ya masuala ya ushirikiano wa kimataifa na sera na makamu wa Rais wa Muungano wa Ulaya pamoja na Dkt. Donald Kaberuka Rais wa zamani wa Benki ya maendeleo barani Afrika na mwenyekiti wa sasa wa bodi ya mfuko wa kimataifa wa kupambana na ukimwi, kifua kikuu na malaria. Na kwamba,“katika miezi miwili ya mwaka 2020 pekee maelfu kwa maelfu ya watu wametawanywa ndani ya nchi zao na kuongeza zaidi idadi ya wakimbizi wa ndani ambao kimataifa sasa ni milioni 41. Wengi wa wakimbizi hawa wamekuwa njiapanda kwa miaka kadhaa baada ya kutawanywa kwa mara ya kwanza wakikosa huduma muhimu kama nyumba, ajira, elimu au mahitaji mengine na fursa.”Katibu Mkuu amelitaka jopo hilo kusaidia kuweka bayana kwa dunia changamoto za wakimbizi wa ndani, kuzitathimini na kuongeza juhudi za kusaka suluhu,

Katibu Mkuu amesisitiza kwamba “haikubaliki kwamba mamilioni ya watu wamefurushwa kutoka majumbani kwao na kisha wanabaki bila suluhu kwa miaka mingi. Kutawanywa haipaswi kuwa zahma kubwa, nina uhakika kwamba jopo hili litaleta mawazo mapya ya kuzuia watu kufurushwa kwa shuruti makwao, kuwalinda, kuwasaidia na kuja na suluhu bora zaidi za watu kutawanywa.”

Kwa upande wake mwenyekiti Bi. Mogherini ameelezea athari kubwa za tatizo la wakimbizi wa ndani na kusisitiza haja ya kusaka suluhu “Madhila yanayosababishwa na watu kutawanywa hasa hivi karibuni Syria, Pembe ya Afrika, DRC na Yemen ni kumbusho kwamba kuna haja ya haraka ya kushughulikia changamoto hii ya wakimbizi wa ndani. Uungaji mkono wa Katibu Mkuu ni muhimu sana wakati tukianza changamoto hii ya kupendekeza njia za kulichukulia tatizo hili na kukabiliana nalo leo.”

Akitambua juhudi ambazo tayari zimeshafanywa kushughulikia upande wa mahitaji ya kibinadamu ya wakimbizi wa ndanni hadi sasa mwenyekiti mwenza Dkt. Kaberuka amesisitiza kwamba juhudi zaidi za kina zinahitajika  “Tunahitaji kubaini miziziya kijamii na kichumi inayosababisha watu kutawanywa ikiwemo umasikini , pengo la usawa, watu kutengwa na kubaguliwa, changamoto za mazingira, za utawala na athari za watu kutawanywa katika kjamii nan chi ili kuweza kupendekeza suluhu sahihi.”