Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola milioni 675 zahitajika ili kuzuia kusambaa kwa virusi vya Corona:WHO

Watu wavaa vinyago vya uso wanapokuwa wakisubiri katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Shenzhen Bao'an nchini China.
UN News/Jing Zhang
Watu wavaa vinyago vya uso wanapokuwa wakisubiri katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Shenzhen Bao'an nchini China.

Dola milioni 675 zahitajika ili kuzuia kusambaa kwa virusi vya Corona:WHO

Afya

Mkurugenzi mkuu wa shirika la afya ulimwenguni WHO, Dkt. Tedross Adhamon Ghebreyesus, leo Jumatano ametoa ombi la dola milioni $675 million ili kupiga jeki  hatua za kimataifa za kukabiliana na mlipuko wa virusi vipya vya Corona wakati idadi ya vifo kutokana na homa hiyo ikikaribia 500.

Akizungumza mjini Geneva Uswis Dkt.Tedros amesema takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kwamba kuna visa 4,363 vilivyothibitishwa nchini China na vifo  490 tangu kutangazwa kwa mlipuko huo Desemba 31 mwaka jana. Ameongeza kuwa “Katika saa 24 zilizopita tumekuwa na visa vingi zaidi katika siku moja tangu kuzuka kwa mlipuko huo. Tuzisahau ni jinsi gani ilivyo vigumu kwa watu wa Wuhan, hivyo kufanya kila liwezekanalo katika sehemu ambayo ni kitovu cha mlipuko huo itasaidia kupunguza kasi ya kusambaa kwa virusi hivyo na hilo ndilo tunalolishuhudia.”

Nje ya China kumeripotiwa visa 191 hadi sasa katika nchi 24 na kumekuwa na kifo kimoja nchini Ufilipino  amesema mkurugenzi huyo wa WHO.

Na kati ya visa hivyo , visa 31 havina historia yoyote ya kusafiri kwenda China lakini vyote vina uhusiano wa karibu na visa vilivyothibitishwa  au mtu aliyetoka kwenye mji ulikoanzia mlipuko huo wa Wuhan.

Fursa ya kukomesha maambukizi ya virusi hivyo

Dkt.Tedross amesisitiza kwamba “Idadi hii ndogo ya maambukizi nje ya China ambako ni maskani ya asilimia 99 ya visa vyote, huku asilimi 80 ya visa hivi vikijikita kwenye jimbo la Hubei pekee  inatoa fursa ya kuzuia mlipuko huo kuwa zahma ya kimataifa .

Amesisitiza kwamba hofu kubwa ya shirika la afya ulimwenguni ni kwamba virusi hivyo vinaweza kufika katika nchi ambazo hazina uwezo wa kubaini maambukizi na hivyo ameitaka jumuiya ya kimataifa kuonyesha mshikamano wa kisiasa, kiufundi na kifedha ili kuhakikisha kwamba mlipuko huo hausambai zaidi.

Hofu yangu kubwa ni kwamba kuna nchi leo hii ambayo hazina mifumo ya kuweza kubaini watu ambao wamepata maambukizi ya virusi hivyo endapo vitazuka. Msaada wa haraka unahitajika kusaidia mifumo dhaifu ya afya kuweza kubaini , kuchunguza na kuhudumia watu waliopata virusi, kiuzuia kusambaa zaidi miongoni mwa binadamu na kuwalinda wahudumu wa afya.”

Tuko imara palipo na udhaifu

Dkt.Tedross ameongeza kuwa “tunakuwa imara tu kama tulivyo na udhaifu, na WHO imetoa dola milioni 9 kutoka kwenye mfuko wake wa ufadhili wa dharura ili kusaidia kukabiliana na mlipuko huo.”

Pia amesema Who limesambaza vifaa 500,000 vya kujikinga na maambukizi pamoja na glovu 350,000, vifaa vya kupumua 40,0000 na mavazi ya wagonjwa 18,000 kwa nchi 24.

Shirika la afya pia limepeleka vipimo 250,000 kwenye maabara zaidi ya 70 kote duniani ili kuharakisha upimaji wa virusi hivyo.”Lakini tunahitaji kufanya zaidi” amesema Tedross kabla ya kuainisha fedha hizo dola milioni 675 zitakavyotumika  katika maandalizi na kukabiliana na mlipuko huo wa Corona hasa katika kuzisaidia nchi kulinda watu wao kwa hatua madhubuti za kujikinga na ufanyaji bvipimo kwa haraka.

“Tunatambua kwamba watu wanahofu na wasiwasi na ni sawa kuwa hivyo,lakini huu sio wakati wa kuogopa, huu sio wakati wa taharuki, ni wakati wa kuchukua hatua kutokana na ushahidi na uwekezaji wakati bado tukiwa na fursa ya kuweza kuudhibiti mlipuko huu.”

Hakuna dawa iliyothibitika kutibu virusi hivyo

Hadi kufikia leo hakuna dawa iliyothibitika kutibu virusi vya Corona Dkt.Michael Ryan mkurugenzi mtendaji wa mpango wa dharura ya afya katika WHOT amewaambia waandishi wa Habari.

Pia amethibitisha kwamba timu ndogo ya wataalam wa kimataifa wa WHO wanatarajiwa kuzuru China ili kujifunza kutoka kwa wataalam wenzao wa huko, na kuongeza kwamba maambukizi hayo yamewakubza zaidi watu wazima waliokuwa na matatizo mengine ya kiafya hapoa kabla.

Amesisitiza kwamba “Kutoa msaada wa kupumua kwa watu walioathirika na mlipuko huo ni muhimu sana “ huku akifafanua kwamba ingawa vifo vingine vimehusihwa pian a viungo vingi vya mwili kushindwa kufanya kazi , wagonjwa mahtuti wanaweza kuishi endapo watapata huduma ya kutosha na ya wakati.

WHO inaamini kwamba mlipuko huo unatoa tishio kubwa zaidi kwa China, na tishio kubwa kikanda na kimataifa. Hatari hiyo imetokana na tathimini ya uwezekano wa kusambaa zaidi, athari zake kwa afya ya binadamu na tofauti ya viwango maandalizi na hatua za kuchukua.

Hivyo wito wa hatua za haraka na za pamoja unaweza kushughulikia hatari hizo kwa mujibu wa WHO na maeneo mengine yanayohitaji msaada.