Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Asilimia 32 ya watu wa zaidi ya miaka 15 Nepali hawajui kusoma wala kuandika:UNESCO

Nchini Nepal na ni taswira ya mji mkuu Kathmandu na kwenye miteremko ya milima ni makazi ya watu na vyanzo vya vipato pamoja na mashamba ya mazao ya chakula
UN Photo/Gill Fickling
Nchini Nepal na ni taswira ya mji mkuu Kathmandu na kwenye miteremko ya milima ni makazi ya watu na vyanzo vya vipato pamoja na mashamba ya mazao ya chakula

Asilimia 32 ya watu wa zaidi ya miaka 15 Nepali hawajui kusoma wala kuandika:UNESCO

Utamaduni na Elimu

Nchini Nepal asilimia 32 ya watu wenye umri wa zaidi ya miaka 15 hawajui kusoma wala kuandika na wanawake na watu wanaoishi vijijini ndio waathirika wakubwa.

Hiyo ni kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO ambalo linasema katika kukabiliana na tatizo hili programu maalum ya uwezeshaji wa maendeleo kupitia elimu (CapED)  imeanzishwa ili kuwasaidia watu hao.

Programu hiyo ni ya kuisaidia serikali ya Nepal kuanzisha mkakati wa kufuta ujinga na elimu ya muda mrefu kupitia sera bora na huduma ya utoaji elimu isiyo rasmi CLC’s ikiwalenga zaidi wanawake na wasichana.

Katika maeneo ambayo ni vigumu kuyafikia CLC’s inatoa fursa za elimu na mafunzo mbalimbali ya ujasiriamali kama ushonaji kwa watu ambao hawajawahi kusoma au walilazimika kukatiza masomo. Na fursa hiyo inatolewa nchi nzima. Bihawana mwenye umri wa miaka 20 ni mmoja wa waliofaidika na mpango huo kwa mafunzo ya ushonaji

(SAUTI YA BIHAWANA SHARMA)

Jina langu Bihawana Sharma baba yangu alikufa nilipokuwa mdogo na mama yangu alifanya kazi kwa bidii ili kutulea na kutusomesha. Nilijiunga na masomo ili niweze kupata kipato kidogo nichangie katika pato letu la familia. Ilinibidi nikope fedha za kulipa karo na kununua vitabu. Sasa sihitaji kuomba kwa wengine naweza kupata kipato change kupitia ushonaji.”

Bihawana hayuko peke yake kuna wanawake na wasichana wengine wengi walio kama yeye

(SAUTI YA KALASHA KADHIKA)

“Nina umri wa miaka 30 , naitwa Kalasha Kadhika Khatri natokea Chingad, sikupata fursa ya kwenda shule katika familia yetu kubwa ya watu 21, ilikuwa vigumu hata kupata milo miwili katika familia kwa siku. Niliolewa mapema katika familia masikini na nilipoteza watoto wawili wadogo. Maisha yalikuwa magumu sikuwa na fedha za kuwatibu ,sikuweza hata kuwapa lishe bora, lakini sasa naweza kuwapa huduma za afya kupitia mradi wangu wa kushona, nimeweka akiba kidogo na ninaweza kumudu gharama za kila siku.”

UNESCO imedhamiria kuhakikisha kwamba programu hiyo inazaa matunda na kusaidia wanawake na wasichana wengi zaidi katika jamii za Nepal.