Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kamishina Mkuu haki za binadamu ahitimisha ziara DRC, atoa wito

Kamishna Mkuu wa Ofisi ya haki za binadamu akizugumza na waandishi habari wakati wa ziara yake Ituri nchini DRC.
MONUSCO
Kamishna Mkuu wa Ofisi ya haki za binadamu akizugumza na waandishi habari wakati wa ziara yake Ituri nchini DRC.

Kamishina Mkuu haki za binadamu ahitimisha ziara DRC, atoa wito

Haki za binadamu

Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet hi leo tarehe 27 Januari amehitimisha ziara yake ya siku tano nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC.

Akihojiwa na Redio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO, kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu ameeleza kuwa kumekuwa na kupungua kwa matukio yaliyoarekodiwa ya vitendo vya ukiukwaji wa haki za binadamu kwa angalau asilimia 3 lakini idadi na ukubwa wa athari kwa jamii bado vinaleta wasiwasi.

Bi Bechelet ametoa wito kwa serikali kuhakikisha inawalinda raia kwani visa vilivyorekodiwa vinaonesha ingawa kwa kiasi vimepungua lakini kiwango bado ni cha juu ikilinganishwa na makundi mengine na kwamba mawakala au tasisi za serikali zinahusika katika utekelezaji na hivyo ushiriki wao katika kuzuia unahitaji.

Aidha Kamishina Bachelet akijibu swali la hatua zinazostahili kupongezwa amesema, “Lakini tunapaswa pia kueleza hatua ambazo zimepigwa katika baadhi ya maeneo, kama uhuru wa kutoa maoni, uhuru wa kukusanyika, kuwaachia wafungwa wa kisiasa ingawa inatakiwa wakati wote kuhakikisha hakuna ukiukwaji wa haki za kisiasa na za kiraia ikiwemo kutokuwepo kushambuliwa kwa wanaharakati watetezi wa haki za binadamu.”

Vile vile Bi Bachelet ameeleza kuwa haki ni msingi wa amani na kwamba njia ya kuelekea kwenye amani itakuwa ngumu na haki haitakuwa endelevu kwa hivyo kunatakiwa kuwa na uwajibikaji.

“Haki inatakiwa kuonekana ikitendeka kwa wale ambao wamekuwa waathirika wakubwa wa makosa na ukikukwaji huo.” Amesisitiza.

Akizungumzia suala la hali mbaya katika magereza nchini DRC, Bi Bachelet ameeleza kusikitishwa kwake na hali alizozisikia kuwa kuna msongamano mkubwa katika magereza, idadi kubwa ya vifo ambayo inahusishwa na  hali mbaya ya usafi na afya na amesema amefanya mazungumzo na Waziri wa wa sheria ambaye ana taarifa hizi na Waziri ataenda katika magereza mbalimbali kuona kinachoweza kufanyika.

“Magereza mapya yanatakiwa kujengwa lakini hilo si jambo unaloweza kulifanya kwa siku moja lakini wataenda katika magereza na kuchambua kesi za waliko huko na kutafuta namna tofauti za kushughulikia haya kwa kuangalia kesi baada ya kesi. Wameniambia wanafahamu kuhusu hili na watatafuta njia za kutatua.” Bi Bachelet amesema.

Katika siku yake ya kwanza nchini DRC, Bi Bachelet alizuru Bunia, mji mkuu wa jimbo la Ituri nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC alhamis ya wiki iliyopita na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya haki za bindamu na wajumbe wa kamati ya usalama wa jimbo hilo ambalo hivi hivi karibuni limegubikwa na changamoto za kiusalama kutokana na mapigano ya kati ya wahema na walendu.

Kaimu gavana wa jimbo hilo Ibrahim Ucircan Bule alimweleza kamishna huyo kuwa wakati mwingine hali ya usalama imekuwa ni chanzo cha ukiukwaji mkubwa wa  haki za binadamu lakini akamshukuru Bi. Bachelet kwa usaidizi wake tangu kuanza kwa janga la ukiukwaji wa haki kwenye jimbo hilo hususan mji wa Djugu tangu mwaka 2017.

Kwa mujibu wa Bwana Bule, vitendo hivyo vya ukiukwaji wa  haki za binadamu vinatekelezwa na kikundi kilichojihami cha Codeco na kusisitiza kuwa juhudi zinafanywa na serikali ya DRC ili kutokomeza ghasia na kwamba kwa upande wa haki, watu kadhaa walikamatwa na kushtakiwa na mahakama ya kijeshi.