Nimestushwa na kusikitishwa na ajali ya ndege Tehran hii leo:UN
Nimestushwa na kusikitishwa na ajali ya ndege Tehran hii leo:UN
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema ameshtushwa na kuhuzunishwa sana kuanguka kwa ndege ya abiria ya Ukrain hii leo Jumatano karibu na mji mkuu wa Iran Tehran.
Kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake hii leo Antonio Guterres ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waathirika wa ajali hiyo na kwa serikali za nchi zote ambazo raia wake walikuwa miongoni mwa abiria waliopoteza maisha.
Kwa mujibu wa duru za Habari ndege hiyo ilikuwa na jumla ya abiria 176 na ilianguka muda mfupi baada ya kuruka kutoka mjini Tehran na kupoteza maisha ya wote waliokuwa ndani.
Abiria na wafanyakazi wa ndege walikuwa wakitoka mataifa mbalimbali ikiwemo Iran, Canada na nchi za Ulaya.
Hivi sasa uchunguzi unaendelea ili kubaini chanzo cha ajali hiyo mbaya na ya kusikitisha.