Mimi ni simulizi ya kupendeza-Doreen Moraa Moracha
Mimi ni simulizi ya kupendeza-Doreen Moraa Moracha
Kuelekea siku ya UKIMWI duniani tarehe Mosi mwezi ujao wa Desemba, Doreen Moraa Moracha, msichana kutoka Kenya ambaye anaishi na virusi vya UKIMWI amekuwa changamoto kubwa katika kumaliza unyanyapaa dhidi ya watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi au VVU.
Doreen amekuwa akifanya hivyo kupitia mitandao ya kijamii na kubwa zaidi katika mahojiano yake na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, UN NEWS Kiswahili anajiita yeye ni simulizi ya kupendeza akisema kuwa, "ninajiita mwenye simuliza ya kupendeza kwa sababu kwa miaka 27 nimekuwa naishi na Virusi Vya Ukimwi, VVU, na nimekuwa kama bingwa kwa sababu niliamua kuwa VVU haviwezi kuwa ndio utambulisho wangu. Na zaidi ya hivyo ni kuonyesha watu ya kwamba kuna maisha zaidi ya vipimo vya VVU. Na ndio maana huwa najiita kuwa ni mwenye simulizi ya kupendeza kwa sababu simuliziyua maisha yangu mwenyewe ni nzuri sana. Kuzaliwa na wazazi ambao mmoja anaishi na VVU na mwingine hana , na kuwa mtoto pekee ninaishi na VVU kwenye familia yangu ni kitu ambacho kinanishangaza hadi inanibidi niseme kuwa nina simulizi ya kupendeza.
Doreen akaulizwa ni upi ujumbe wake kwa jamii, na hakusita kusema ya kwamba, "jamii ina nafasi k ubwa sana katika k utupilia mbali unyanyapaa kwa vile zile dhana potofu ambazo tumekuwa nazo kuhusu VVU zimetokana na jamii. Jamii ni lazima ielimishane kuwa kuwa na VVU si hukumu ya kifo na kwamba watu wanaoishi na VVU ni binadamu kabla ya vile virusi tunavyoviona. Ni vizuri tuanze kuangalia binadamu kabla ya kuangazia VVU. Na hii yote itatokana na jamii kwa vile ni jamii yenyewe ilianzisha dhana kuwa watu wanaoishi na VVU ni watu waliokonda, wana wapenzi wengi na watu ambao tabia zao kwenye jamii si za kisawasawa. Kwa hivyo ni jamii irudi pale ilipoanzia ianze kuzungumzia suala hilo.