Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nasaidia wengine kama nilivyosaidiwa miaka 40 iliyopita-Mshindi wa tuzo ya Eleanor Roosevelt

Chris Mburu, mshindi wa tuzo ya haki za binadamu ya mwaka 2019 ya Eleanor Roosevelt, katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, New York Marekani. (19 Novemba 2019)
UN News/Anold Kayanda
Chris Mburu, mshindi wa tuzo ya haki za binadamu ya mwaka 2019 ya Eleanor Roosevelt, katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, New York Marekani. (19 Novemba 2019)

Nasaidia wengine kama nilivyosaidiwa miaka 40 iliyopita-Mshindi wa tuzo ya Eleanor Roosevelt

Haki za binadamu

Waswahili wanasema tenda wema nenda zako na pia wema hauozi. Mwezi huu tuzo ya haki za binadamu ya Eleanor Roosevelt imeenda kwa mtu ambaye miaka 40 iliyopita alikuwa mtoto maskini asiye na matumaini ya kuendelea kukanyaga darasani licha ya ufaulu wake kuwa mzuri.

Chris Mburu, akihojiwa na Priscilla Lecomte wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anaeleza sifa zilizofanikisha kumpa tuzo hiyo ambayo hutolewa kila mwaka kwa watetezi bora wa haki za binadamu.

“Hiyo tuzo nimepewa kwasababu wameangalia  ile kazi ambayo nimekuwa nikifanya katika Umoja wa Mataifa lakini kwa kazi yangu ya binafsi ya chama nilichoanzisha huko kwetu Kenya cha kusaidia watoto ili wasome kwasababu mimi nimesomeshwa na mtu ambaye alinionea huruma akanisomesha. Kwa hivyo baadaye  nilianzisha chama ambacho kina jina la yule mwanamke kutoka Sweden ambaye alinisaidia.” Bwana Mburu Anafafanua.

Eleanor  Roosevelt wa Marekani akiwa ameshikilia nyaraka yenye tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa katika picha hii ya Novemba 1949
UN
Eleanor Roosevelt wa Marekani akiwa ameshikilia nyaraka yenye tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa katika picha hii ya Novemba 1949

Na kuhusu ni nini kilimfanya aishi kwa kutegemea misaada Anaeleleza, “mimi nilizaliwa katika familia maskini katika kijiji kinachoitwa Mitahato huko mkoa wa kati nchini Kenya. Na wakati ule elimu ilikuwa ya kulipia na familia yetu ikapata shida na mama yangu akatafuta msaada kwa wageni ambao walikuwa wanajihusisha na  elimu ya watoto. Basi niliunganishwa na mwanamke mmoja kutoka Sweden ambaye anaitwa Hilde Back, sasa yule mama ndiye alinisomesha kuanzia shule ya msingi, ya sekondari na baadaye nikaenda chuo kikuu cha  Kenya kusomea sheria  na kisha chuo kikuu cha Harvard nchini Marekani. Na nimefurahi sana vile alivyonifanyia hata ndiyo maana nikasema chama changu kitakuwa n ajina lake yaani Hilde Back Education Fund  na tunawasaidia watoto ambaao wako katika ile hali ambayo nilikwemo miaka arobaini iliyopita.”