Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kebehi, matusi, makaripio vyakumba wajawazito wakati wa kujifungua- Utafiti

Mkunga na mama mjamzito
Photo: WHO/A. Esiebo
Mkunga na mama mjamzito

Kebehi, matusi, makaripio vyakumba wajawazito wakati wa kujifungua- Utafiti

Afya

Utafiti mpya wa Shirika la afya ulimwenguni, WHO, unaonesha kwamba theluthi moja ya wanawake katika nchini 4 za kipato cha chini wameripoti kukumbwa na mateso wakati wa kujifungua.

Takwimu hizo ni kwa mujibu wa utafiti uliofanyika kwenye mataifa menne ambayo ni Ghana, Guinea, Myanmar na Nigeria ikuhusisha wanawake 2,016 na matokeo yake kuchapishwa kwenye jarida la afya la Lancet.

Matokeo ni kwamba asilimia 42 ya wanawake hao walikumbwa na ukatili wa kimwili na kimaneno, kunyanyapaliwa na kubaguliwa wakati walipokuwa wameshikwa na uchungu.

WHO inasema msaada kutoka kwa mkunga wakati mjamzito anajifungua unaweza kuwa na mchango kati ya uhai na kifo na kwamba huduma za mkunga zimeonesha kupunguza vifo vya mama na mtoto na watoto njiti kwa asilimia 80, na kupunguza uchungu wa kabla ya kutimia muda wa kujifungua kwa asilimia 80.

Hata hivyo, takriban wanawake 800 hufariki kila siku wakati wa uchungu wa kujifungua.

Utafiti umetanabaisha kwamba wanawake wenye umri mdogo, na walio na kiwango cha chini cha elimu wako hatarini kuteswa kupitia kunyanyapaliwa, kubaguliwa, kufanyiwa taratibu za kitabibu bila ya hiari yao, kutelekezwa au kutofutiliwa na wahudumu wa afya.

Tweet URL

Takriban asilimia 14 ya wanawake walikumbwa na aina fulani ya ukatili wa kimwili ikiwemo kupigwa vibao, kupigwa ngumi huku wengine wakifanyiwa upasuaji wa kujifungua bila ya idhini yao au kuongezwa njia wakati wa kujifungua kwa njia ya kawaida na kukaguliwa sehemu za siri.

Utafiti pia umefanyika kwa wanawake 2,672 baada ya kujifungua, ambao umeonesha viwango vya sawa vya mateso.

Watafiti waligunudua kwamba visa 35 vya uzalishaji kupitia upasuaji vilitokea bila ya idhini ya mama sambamba na visa 190 kati ya 253 vya kuongezwa kwa njia na utafiti 2,611 vya ufuatiliaji wa ikiwemo asilimia 59 ya idadi yote.

Takriban wanawake 752 sawa na asilimia 38 waliotafitiwa walieleza kupitia aina moja ya nyingine ya matusi iwe ni kukemewa, kukaripiwa na kukejeliwa. Wanawake walikuwa ni wahanga wa ubaguzi na unyanyapaa kwa misingi ya rangi au kabila.

Mikakati ya kuzuia

WHO imependekeza baadhi ya mikakati kuhakikisha kwamba wanawake wanapata huduma kwa njia ya huruma na utu kuanzia kuwajibisha mifumo ya afya hadi kuhakikisha kwamba kuna raslimali za kutosha kwa ajili ya huduma bora ya afya na sera zinazojali haki za wanawake ikiwemo.

Rasilimali hizo ni pamoja na kutengeneza vyumba vya kujifungua kwa kuzingatia mahitaji ya wanawake, kuimarisha mchakato wa kutoa idhini kuhusu hatua za kitabibu, kuimarisha uwezeshaji na msaada kwa wahudumu wa afya kuimarisha viwango vya huduma.

Halikadhalika kuruhusu wanawake wote kuwa na mtu wakati wa uchungu na wa kujifungua, kusisitiza umma kutaka huduma bora za uzazi ambayo haina nafasi ya kuteswa au ukatili, WHO imechagiza makundi ya tasnia kuungana kuchagiza na kuunga mkono huduma bora miongoni mwa wahudumu wa wafya ya uzazi na wakunga na wanaohudumia wanawake wajawazito.

Mwaka jana, WHO ilipendekeza mambo kadhaa katika huduma ya mama wakati wa ujauzito na wakati wa kujifungua kwa kuzingatia mbinu zinazojali mwanamke.

Sehemu muhimu ya WHO kuchagiza afya kwa wote ni kuendeana na afya ya mama na mtoto kwa kuzingait lengo namba tatu la malengo ya maendeleo endelevu ya kuhakikisha Maisha yenye afya na uzima kwa wote.