Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Rwanda, UNHCR na Muungano wa Afrika wakubaliana kuhamisha wakimbizi kutoka Libya

Picha ya maktaba ikionesha afisa wa IOM akikagua nyaraka za wahamiaji kutoka Nigeria kabla ya kupanda Basi kurejea kwao wakitokea Libya.
IOM/Marian Khokhar
Picha ya maktaba ikionesha afisa wa IOM akikagua nyaraka za wahamiaji kutoka Nigeria kabla ya kupanda Basi kurejea kwao wakitokea Libya.

Rwanda, UNHCR na Muungano wa Afrika wakubaliana kuhamisha wakimbizi kutoka Libya

Wahamiaji na Wakimbizi

Serikali ya Rwanda, Shirika la Kuhudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa, UNHCR na Muungano wa Afrika, AU leo hii wametia saini makubaliano ya kuanza mchakato wa kuhamisha wakimbizi kutoka Libya. 

Chini ya makubaliano hayo, serikali ya Rwanda itawapokea na kuwapa ulinzi wakimbizi na waomba hifadhi ambao kwa sasa wanazuiliwa katika vituo vya kuwazuilia nchi Libya. Watahamishwa kwenda Rwanda kwa hiari.

Kundi la kwanza la watu 500, wengine kutoka Pembe ya Afrika watahamishwa, wakiwemo watoto na vijana walio hatarini. Baada ya kuwasili UNHCR itaendea kuwahudumia wakiambizi hao.

Huku baadhi wakiwa watanufaika kwa kupewa makao katika nchi zingine, wengine watasaidiwa kurudi nchini ambapo hifadhi zilikuwa zimetolewa awali, au warudi nchi zao kama itakuwa salama kufanya hivyo. Wengine wataruhusiwa kusalia Rwanda kwa makubaliano na mamlaka husika.

Safari za kuwahamisha zinatarajiwa kuanza wiki zinazokuja na zitafanywa kwa ushirikiano kati ya mamlaka za Rwanda na Libya. UNHCR itatoa huduma za ulinzi na pia misaada ya kibinadamu ikiwemo chakula, maji, makao, elimu na huduma za afya.

UNHCR inatoa wito kwa jamii ya kimataiafa kutoa mchango kusaidia kutekelezwa makubaliano hayo. UNHCR imehamisha zaidi ya wakimbizi 4,400 na watafuta hifadhi kutoka Libya kwenda nchi zingine tangu mwaka 2017 wakiwemo 2,900 kupitia njia ya dharurua huko Niger na 425 kwenda nchi za Ulaya kupitia Romania.

Lakini takriban watu 4,700 kwa sasa wanakadiriwa kuzuiliwa katika mazingira duni kwennye vizuizi nchini Libya. Wanahitaji kuhamishwa kwa dharura na kupewa ulinzi na kupata suluhu ya kudumu.