Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

FAO yaonya kuhusu mlipuko wa nzige wa jangwani Yemen na pembe ya Afrika

Nzige wa jangwani.
Picha: FAO/G.Tortoli
Nzige wa jangwani.

FAO yaonya kuhusu mlipuko wa nzige wa jangwani Yemen na pembe ya Afrika

Masuala ya UM

Shirika la chakula na kilimo FAO leo limetoa onyo dhidi ya mlipuko wa nzige wa jangwani katika eneo la Pembe ya afrika na Yemen, likisema nzige hao waliochochewa na mvua kubwa wanaweza kuwa tishio kubwa kwa uzalishaji wa kilimo katika miezi mitatu ijayo.

Kwa mujibu wa shirika hilo maeneo yaliyo hatarini zaidi ni Yemen, Sudan, Eritrea na baadhi ya sehemu za Ethiopia na Kaskazini mwa Somalia. Limeongeza kuwa “hali hiyo inaweza kusababisha athari kubwa katika mazao ya msimu wa kilimo na uchumi wa maeneo hayo kitu ambacho ni tisho la uhakika wa chakula  na Maisha ya watu wan chi husika.

FAO inasema mwaka huu operesheni kubwa zimeendeshwa kuzuia zahma kama hiyo kwa nchi za Iran, Saudia, na Sudan na kwa kiasi kikubwa zimesaidia kupunguza idadi ya nzige hao  ingawa haikuweza kuwazuia kabisa kuelekea maeneo mengine ambako huathirika wakati huu wa kiangazi yakiwemo Yemen, Sudan, Pembe ya afrika na pande zote za mpaka wa Pakistan.

Endappo nzige hao hawatodhibitiwa FAO inasema kuna hatari ya wastani ya hali ya nzige wa jangwani kuongezeka zaidi katika maeneo ya ndani na pwani ya Yemen na maeneo ya vijijini ya Sudan, na kusababisha kuundwa kwa mapango ambayo yatatishia uzalishaji wa kilimo mwishoni mwa msimu wa joto.

Hii itafuatwa na kuongezeka zaidi pande zote mbili za bahari ya Shamu wakati wa msimu ujao wa baridi kuanzia Novemba kuendelea.