Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mradi wa UNICEF wa vitabu za kidijitali zatoa fursa kwa watoto wanoishi na ulemavu Kenya

Wanafunzi wakitumia kompyuta mpakato katika mraddi wa shule wa (INS) kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya. Mradi wa INS ni wa ushirikiano baina ya UNHCR na wakfu wa Vodafone.
UNHCR/Catherine Wachiaya
Wanafunzi wakitumia kompyuta mpakato katika mraddi wa shule wa (INS) kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya. Mradi wa INS ni wa ushirikiano baina ya UNHCR na wakfu wa Vodafone.

Mradi wa UNICEF wa vitabu za kidijitali zatoa fursa kwa watoto wanoishi na ulemavu Kenya

Utamaduni na Elimu

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF na wadau wamezindua jaribio la kitabu cha kidijitali katika shule 25 za msingi  nchini Kenya kwa lengo la kuimarisha elimu ya kidijitali hususan kwa watoto walio hatarini au maeneo ya vijijini au mitaa ya mabanda na wanaoishi na ulemavu. 

Kupita video ya UNICEF tunakutana na mwanafunzi wa shule ya msingi akiwa darasani amevalia sare ya shule ambayo ni sweta ya kijani na shati jeupe. Kwenye dawati ana kompyuta ndogo kwa makini kabisa anafuata maelekezo kupitia lugha ishara.

UNICEF imesema watoto wengi walio na ulemavu wa viungo mara nyingi wanakosa elimu kwa sababu ya kukosa vifaa elimu lakini vitabu mtandaoni ni habari njema. 

Vitabu hivi vinahakikisha kwamba watoto walio na ulemavu wa kuona wanapata vitabu hivyo kwa njia ya sauti na lugha nyepesi kwa walio na ulemavu wa upungufu wa kuelewa pia lugha ishara kwa viziwi. 

Mfumo huu unakaribishwa pia na walimu kama anavyosema mwalimu Martha Mwango kutoka shule ya msingi ya Aga Khan ambaye anaonekana na wanafunzi wake darasani

(Sauti ya Martha)

“Mfumo wa kidijitali wa kusoma ni mzuri sana kwa viziwi, ni wazo zuri ambalo tunalitekeleza kwa sababu wanafunzi hawa wanatumia uwezo wao wa kuona wakati wanasoma na vitabu vya kidijitali vina picha, ishara na rangi kwa hiyo inawatia moyo sana.”

Mfumo huu umetajwa kuwa muhimu katika kuhakikisha kwamba wanafunzi wanakwenda sambamba na wenzao wasio na ulemavu wa viungo kwani katika zama za sasa teknolojia inatumika katika mambo mbali mbali.

Kwa upande wao wanafunzi ambao walikuwa wamezoea mfumo wa kizamani wa mafunzo sasa wanapata taswira kamili kwani wanajifunza kupitia picha na video. Mwanafunzi Keith kupitia lugha ishara anasema, “nimependa sana kitabu hiki, ninafurahi kukisoma, ninapenda picha na kusoma hadithi zilizomo.”