Kutoa ni moyo, mkimbizi asaidia wakimbizi wenzake na wenyeji
Kwa msaada wa UNHCR, mkimbizi, mmoja kutoka Syria, hivi sasa anafanya mafunzo ya sanaa, bila malipo nchini Misri kupambana na masuala kama vurugu, kiwewe cha vita, unyanyasaji wa kingono na ubaguzi wa rangi.
Nchini Syria, Bassem alikuwa muongozaji wa Sanaa za jukwaani. Baada kukimbilia Misri akapata wazo la kuwakutanisha vijana ambao wamekumbwa na madhila katika jamii zao.
(Sauti ya Bassem)
“Vijana wadogo wa Syria wanaofika hapa wamepatwa na kiwewe. Kujaribu kuwafanya warejee katika hali nzuri tunatakiwa kuwapa Sanaa na vichekesho, kitu ambacho kinawafanya wacheke na kuendeleza vipaji vyao.”
Zaidi ya robo tatu ya wanafunzi wa Bassem ni raia wa Misri
(Sauti ya Bassem)
“kila kitu kilianza na wazo la kuwaleta pamoja vijana. Kisha kijana mmoja Mmisri akajiunga. Nililipenda wazo kisha nikawaza kwa nini nisitengeneze dhamira ya kujumuika pamoja? Kwa hivyo nikawaleta wasyria na wamisri pamoja, baadaye wayemeni, wairaq na wasudani wakajiunga. Kwa hivyo tukaanzisha hili kundi.”
Hazem, raia wa misri ni msaidizi wa Bassem anasema,
(Sauti ya Hazema)
“tabia yangu ilibadilika kwasababu yake. Nilipojiunga na timu nilikwepa kuongea na yeyote. Lakini alinisaidia kushirikiana na wengine.”
Bassem pia anajifunza kutoka kwa wanafunzi wake na anaona sanaa ni njia ya kuelekea kwenye amani na kuishi pamoja.