Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

IOM na Japan wapiga jeki juhudi za kuzuia magonjwa

Manusura wa majanga ya asili, jimbo la Rumonge nchini Burundi- Novemba 28 2018
Picha: OCHA Burundi / Ana Maria Pereira
Manusura wa majanga ya asili, jimbo la Rumonge nchini Burundi- Novemba 28 2018

IOM na Japan wapiga jeki juhudi za kuzuia magonjwa

Afya

Shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji, IOM na serikali ya Japan wamezindua mradi wa pamoja kwa mwaka mmoja kwa ajili ya kusaidia watu wanaokabiliwa na milipuko ya magonjwa, majanga ya asili na wanaorejea nchini Burundi.

Uzinduzi wa mradi huo umeendana sambamba na msaada wa dola milioni moja za kimarekani kutoka kwa Japan kwa ajili ya kuimarisha uwezo wa mamlaka ya kitaifa na jamii mashinani ambazo zitasaida katika kuzuia na kukabilliana na milipuko ya mogonjwa kwenye mipaka.

Kwa mujibu wa taarifa ya IOM, nchi maskini kama Burundi pindi kunapotokea mvua za msimu husababisha watu kufurushwa kwa ajili ya mafuriko na mmomonyoko wa udongo ambavyo vyote vinaathiri wakulimwa wadogo wadogo na wafanya biashara ndogo ndogo wengi wao wakiwa katika hatari ya kupoteza shamba zao na mifugo wakati majanga hayo yakitokea huku yakifuatana na milipuko ya magonjwa na dharura zingine za kiafya.

Makadirio ya IOM nchini Burundi yanaonyesha kwamba majanga ya asili husababisha takriban asilimia 77 ya visa vya kufurushwa huku nchi hiyo inayopakana na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Rwanda na Tanzania ikihitaji miundombinu na vifaa zaidi ikiwemo kwa ajili ya kufuatilia hali ya kiafya kwenye mipaka. 

Wakati huu kunashuhudiwa mlipuko wa ebola katika nchi jirani, DRC ikijumuishwa na hatari za usambaaji wa magonjwa mpakani kunahatarisha kutpkea janga ikizingatiwa kwamba majimbo tisa kati ya 18 ya Burundi yanapakana na nchi jirani.