Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto 19 wauawa Sudan ndani ya wiki moja, UNICEF yapaza sauti

Umati wa watu wakianadamana kwenye mitaa ya mji mkuu wa Sudan Kharthoum 11 Aprili 2019
PICHA:Ahmed Bahhar/Masarib
Umati wa watu wakianadamana kwenye mitaa ya mji mkuu wa Sudan Kharthoum 11 Aprili 2019

Watoto 19 wauawa Sudan ndani ya wiki moja, UNICEF yapaza sauti

Amani na Usalama

Takriban watoto 19 wamearipotiwa kuuawa nchini Sudan na wengine 49 kujeruhiwa tangu Juni 3 mwaka huu amesema mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa kuhudumia watoto UNICEF.

Bi Henrietta fore katika taarifa yale iliyotolewa leo amesema “Ninatiwa hofu kubwa na athari za kuendelea kwa vita na machafuko nchini Sudan kwa watoto na vijana hususan taarifa zinazoripotiwa za matumizi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya wanaoandamana kwa amani.”

Fore ameongeza kuwatumepokea taarifa kwamba Watoto wanashikiliwa kizuizini, wanaingizwa kushiriki vitani na kufanyiwa ukatili wa kingono. Shule, hospitali na vituo vya afya vinalengwa na mashambulizi, kuporwa na kuharibiwa. Wahudumu wa afya wamekuwa wakishambuliwa kwa sababu tu ya kutimiza wajibu wao , wazazi wengi wanahofu kubwa ya kuwaacha watoto wao watoke nje ya nyumba zao, wanahofia machafuko, udhalilishaji na kutozingatiwa kwa sheria.”

Taarifa hiyo ya Bi. Fore iliyotolewa Jumanne imeendelea kusema kwambakumeripotiwa upungufu mkubwa wa maji, chakula na madawa katika nchi nzima hali inayoweka rehani afya za watoto na mustakbali wao. Amesisitiza kuwa watoto Sudan nzima tayari wanabeba mzigo mkubwa wa miongo ya vita, maendeleo duni na uongozi mbovu na machafuko ya sasa yanaifanya hali mbaya kuwa mbaya zaidi.”

Msichana mwenye umri wa miaka 12  akiyebakwa na vikosi vya wanajeshi Sudan
UN
Msichana mwenye umri wa miaka 12 akiyebakwa na vikosi vya wanajeshi Sudan

Hata katika machafuko ya sasa amesema kazi ya UNICEF katika kulinda mustakabali wa watoto nchini Sudan inaendelea “Tunawasaidia mamilioni ya watoto wakiwemo wale waliotawanywa au wakimbizi kwa kuwapa chanjo, maji safi, tiba ya utapiamlo uliokithiri na msaada wa kisaikolojia, lakini machafuko ni lazima yakome.”

UNICEF imetoa wito kwa pande zote zinazohusika katika mzozo kulinda watoto kwa wakati wote na kuwaepusha na athari za machafuko hayo, ikisema mashambulio yoyote dhidi ya watoto, shule au hospital ni ukiukwaji mkubwa wa haki za watoto.

UNICEF pia imeitolea wito mamlaka ya Sudan kuruhusu mashirika ya misaada ya kibinadamu kuwafikia wanaohitaji msaada ikiwa ni pamoja na fuesa za kufika hospital ambazo zimekuwa zikizuiliwa au kufungwa.

Bi. Fore amesisitiza kwamba “Naungana na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuzitaka pande zote kusaka suluhu kwa njia ya majadiliano na kuanza mazungumzo ya amani kuhusu kuhamishia madaraka katika utawala wa kiraia.watoto wa Sudan wanataka amani, na jumuiya ya kimataifa inahitaju kuchukua msimamo wa kusaidia matarajio haya.”