Usafiri wa baiskeli una faida za kiafya isitoshe kimazingira

Mahitaji ya wasafiri ambao hutembea kwa miguu au kuendesha baiskeli, ambayo ni idadi kubwa ya watu yanapuuzwa na mataifa mengi licha ya kwamba faida za kuwekeza katika usafiri wa kundi hili zinaweza kuokoa maisha, kusaidia kulinda mazingira na kupunguza umaskini.
Kauli hiyo ni kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa katika ujumbe wake wa kuadhimisha siku ya baiskeli duniani ambayo kila mwaka huadhimishwa Juni 3.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo kwa ajili ya siku hii kushughulikia mahitaji ya waendesha basikeli na wanao tembea kwa miguu ni muhimu katika suluhu za usafiri na kusaidia miji kuimarisha hali ya hewa na usalama barabarani.
Shirika la afya ulimwenguni, WHO limesema mazingira salama ya kutembea na kuendesha baiskeli ni suala muhimu katika kufikia usawa wa kiafya kwani kwa watu maskini ambao hawana magari, kutembea na kuendesha baiskeli kunawapa mfumo wa usafiri ambao unapunguza hatari za kupata magonjwa ya moyo, baadhi ya saratani, kisukari na hata kufariki dunia na hivyo sio tu kuna faida za kiafya lakini pia gharama zake ni nafuu na rafiki.
Mbali na gharama zake, matumizi ya baiskeli ni safi na yanajali mazingira na kwa hiyo ni usafiri endelevu. Aidha baiskeli inaweza kutumika kwa ajili ya kuimarisha elimu, afya na michezo. Pia matumizi ya baiskeli yanachagiza ujumbe chanya kwa ajili ya matumizi endelevu na uzalishaji ambao hauna athari mbaya zinazochangia mabadiliko ya tabianchi.