UN yachukua hatua Msumbiji kukabili madhara ya kimbunga Kenneth
UN yachukua hatua Msumbiji kukabili madhara ya kimbunga Kenneth
Kimbunga Kenneth kikitarajiwa kupiga maeneo ya kaskazini mwa Msumbiji jioni ya leo siku ya Alhamisi, Umoja wa Mataifa nchini humo umesema tayari umeanza kuchukua hatua ili kupunguza madhara ya kimbunga hicho ambacho pia kinatarajiwa kupiga maeneo ya kusini mwa Tanzania.
Mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Msumbiji Marcoluigi Corsi, ameiambia Idhaa ya Umoja wa Mataifa kuwa, “kile ambacho tumefanya hadi sasa kama UN ni kuhamasisha timu yetu kwenye mji mkuu wa jimbo la Cabolgado, Pemba ambayo inafanya kazi kwa ushirikiano na mamlaka za mitaa na kitaifa na tumeweka vifaa vya misaada vitakavyotumika kusaidia wilaya zitakazoathirika.”
Mapema Filipe Lucio kutoka mradi wa huduma za tabianchi WMO amesema ni vyema kuchukua hatua za dharura kwa kuwa kimbunga hicho kitaambatana na upepo wenye kasi ya kati ya kilometa 130 kwa saa hadi kilometa 180 kwa saa huku kiwango cha mvua kikitarajiwa kuwa kati ya meta 2 hadi 4 kutoka usawa wa ardhi.
Huku mamlaka hizo zikichukua hadhari, Bwana Lucio amesema, “ni kuelimisha umma kuhusu madhara ambayo kimbunga Kenneth kinaweza kusababisha. Lakini pia hatua za kuchukua kama vile kwenye miundombinu na makazi mbadala kwa watu ambao nyumba zao si imara. Upepo wa kasi ya kilometa 180 kwa saa unaweza kuzibomoa, kwa hiyo mawasiliano hayo lazima yafanyike kwa watu walio hatarini ili waweze kuchuka hatua.”
Bwana Lucio amesihi wakazi wa maeneo hayo wasichelee kuchukua hatua kwa kuwa kimbunga kinakuja na hatua zianze sasa ili wawe tayari pindi kimbunga kitakapopiga.
Mwezi uliopita kimbunga Idai kilipiga majimbo manne ya Msumbiji na kusababisha madhara makubwa ya uhai wa binadamu, mali na miundombinu.