Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Notre Dame ikiteketea,UN yapaza sauti

Moto ukiteketeza kanisa kuu la kale la Notre Dame mjini Paris, Ufaransa. Moto huu ulianza wakati ukarabati wa kanisa hilo ukiendelea leo tarehe 15 Aprili 2019
Katie Dallinger
Moto ukiteketeza kanisa kuu la kale la Notre Dame mjini Paris, Ufaransa. Moto huu ulianza wakati ukarabati wa kanisa hilo ukiendelea leo tarehe 15 Aprili 2019

Notre Dame ikiteketea,UN yapaza sauti

Utamaduni na Elimu

Mjini Paris, Ufaransa wingu zito la moshi limetanda angani wakati huu ambapo kanisa kuu la kale mjini humo, Notre Dame linateketea kwa moto.

Vyombo vya  habari vinaripoti kuwa moto huo ulioanza saa 12.30 jioni kwa saa za Ufaransa leo Jumatatu tayari umeporomosha  mnara mkuu wa kanisa hilo lililojengwa kuanzia mwaka 1163 hadi mwaka 1345.

Hadi sasa askari wa zimamoto wanaendelea kuhaha kudhibiti moto huo ambao chanzo chake bado hakijafahamika.

Tweet URL

Kufuatia tukio hilo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ukurasa wake wa Twitter amesema, “ nimeshtushwa na picha zinazotoka Paris zikionesha moto unateketeza kanisa kuu la Notre Dame, mfano wa kipekee wa urithi wa dunia ambao umesimama imara tangu karne ya 14.”

Katibu Mkuu amesema kuwa fikra zake hivi sasa zipo na wananchi na serikali ya Ufaransa.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO Audrey Azoulay amesema kupitia ukurasa wake wa Twitter kuwa hisia kubwa zimezingira watu wanaoshuhudia kuungua moto kwa kanisa hilo ambalo UNESCO ililiorodhesha kama urithi wa dunia mwaka 1991.

“UNESCO inafuatilia kwa karibu hali ilivoy na ikon a mshikamano na Ufaransa ili kulinda na kukarabati urithi huo wa aina yake,” amesema Bi.Azoulay.