Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto ni waathirika wakubwa mwezi mmoja tangu kimbunga Idai-UNICEF

Mtoto wa umri wa miaka 6 akiwa ameshika kabrasha lake la elimu alilolipokea kutoka UNICEF ikiwa ni sehemu ya msaada wa watoto na familia zilizoathiriwa na kimbunga Idai nchini Msumbiji.
UNICEF/James Oatway
Mtoto wa umri wa miaka 6 akiwa ameshika kabrasha lake la elimu alilolipokea kutoka UNICEF ikiwa ni sehemu ya msaada wa watoto na familia zilizoathiriwa na kimbunga Idai nchini Msumbiji.

Watoto ni waathirika wakubwa mwezi mmoja tangu kimbunga Idai-UNICEF

Msaada wa Kibinadamu

Mwezi moja tangu kimbunga Idai kukumba nchi za Msumbiji, Malawi na Zimbabwe, Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, limetoa ombi la dola milioni 1.6 kusaidia watoto ambao wanaibuka kutoka athari zake mwezi mmoja tangu kimbunga hicho.

Akizungumza kuhusu hali ya watoto baada ya kimbunga hicho mkurugenzi mkuu wa UNICEF, Henritta Fore ambaye alizuru Msumbiji pindi tu baada ya kimbunga hususan katika mji wa Beira amesema, “watoto wanaoishi katika makazi yaliyojaa watu mbali na makazi yao wako hatarini ya magonjwa, kutumikishwa na ukatili.”

UNICEF imesema watoto milioni moja nchini Msumbiji, 443,000 nchini Malawi na 130,000 nchini Zimbabwe wana mahitaji makubwa ikiwemo huduma ya afya, lishe, elimu na maji.

Tangu kimbunga hicho kupiga Msumbiji, visa vya kipindupindu vimeiongezeka kufikia hadi 4,600 huku visa vya malaria vikifika 7,500.

UNICEF imesema kusitishwa kwa huduma muhimu huenda kukasababisha mlipuko wa magonjwa na ongezeko la utapiamlo ambapo watoto wako hatarini.

Kwa mantiki hiyo Bi. Fore amesema, “barabara kuelekea kupona, itakuwa ndefu na ni muhimu kwa washikadau wa misaada ya kibinadamu wahusike katika kila hatua.”

Kwa mujibu wa UNICEF, takriban nyumba 200,000 ziliharibiwa nchini Msumbiji tu na kwa sababu kimbunga hicho kilitokea wiki chache tu kabla ya mavuno, uhakika wa chakula uko njia panda.

Wakati huo huo, maelfu ya watu wanasalia katika kambi za muda mfupi ambapo UNICEF imeelezea wasiwasi wake kuhusu hatma ya watoto takriban 130,000 waliolazimika kuhama nchini Musumbiji na Malawi.

UNICEF imesisitiza umuhimu wa kusaidia watoto na familia kukabiliana na hali ya sasa na kurejelea katika maisha yao hapo baadaye.

UNICEF imetoa ombi la dola milioni 122 kwa ajili ya kusaidi watoto na familia walioathirika na kimbunga na athari zake nchini Msumbiji, Zimbabwe na Malawi kwa kipindi cha miezi tisa ijayo.