Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mapinduzi ya kidijitali yasaidia kuinua uchumi wa baadhi ya nchi Afrika- Ripoti

Malipo ya miamala kwa njia ya kidijitali yanatumika sasa kuinua uchumi wa nchi mbalimbali duniani ikiwemo Afrika
Benki ya Duniak/Simone D. McCourtie
Malipo ya miamala kwa njia ya kidijitali yanatumika sasa kuinua uchumi wa nchi mbalimbali duniani ikiwemo Afrika

Mapinduzi ya kidijitali yasaidia kuinua uchumi wa baadhi ya nchi Afrika- Ripoti

Ukuaji wa Kiuchumi

Ripoti mpya ya Benki ya Dunia kuhusu uchumi kwa nchi za Afrika zilizo Kusini mwa jangwa la Sahara inasema kuwa ukuaji uchumi kwa nchi hizo umeendelea kuwa chini kwa mwaka wa nne mfululizo ikilinganishwa na ongezeko la idadi ya watu ingawa kiwango cha ukuaji uchumi kwa eneo hilo kwa mwaka huu wa 2019 kinatarajiwa kuwa ni asilimia 2.8.

Takwimu hizo ni kwa mujibu wa ripoti mpya ya Benki ya Dunia iitwayo Pulse ambayo hupima hali ya chumi za Afrika mara mbili kwa mwaka.

Mathalani ripoti imesema kwa sababu za ndani na nje ya nchi hizo, kiwango cha ukuaji kwa mwaka jana kimelazimika kupunguzwa hadi asilimia 2.3 kutoka asilimia 2.5 mwaka uliotangulia wa 2017.

Mchumi Mkuu wa Benki ya Dunia kwa nchi za Afrika Albert Zeufack, akizungumzia ripoti hiyo amesema kasi ndogo inaakisi ukosefu wa uhakika kwenye uchumi wa dunia lakini “ndani ya nchi, ukosefu wa uhakika wa uchumi mkuu ikiwemo ongezeko la usimamizi dhaifu wa madeni, nakisi ya fedha na mfumuko wa bei vimeshamiri kwenye mataifa mengi na vinaathiri uchumi wa Afrika. Zaidi ya yote hali  ya utete inakwamisha ukuaji wa nchi za Afrika.”

Pengo la teknolojia ya dijitali bado ni kikwazo duniani.
ITU
Pengo la teknolojia ya dijitali bado ni kikwazo duniani.

Zambia imetajwa kuwa miongoni mwa nchi ambazo udhibiti dhaifi wa madeni unarudisha nyuma uchumi ilhali Angola nayo hali si shwari kutokana na kudorora kwa uzalishaji wa mafuta.

Hata hivyo nchi zisizo na rasilimali nyingi kama vile Kenya, Rwanda na Uganda zimeibuka kidedea kwa kiwango cha juu cha ukuaji uchumi kwa mwaka 2018 ambapo Bwana Zeufack anasema, “mapinduzi ya kidijitali yanaweza kufungua fursa mpya za ukuaji jumuishi na fursa za ajira Afrika. Ni kwamba ripoti yetu hii mpya imebaini manufaa ya uchumi wa kidijitali ni dhahiri kwa nchi za Afrika zilizo kusini mwa jangwa la Sahara. Yanaweza kuongeza karibu asilimia 2 kwenye pato la taifa kila mwaka au kupunguza umaskini kwa karibu asilimia 1 kwa mwaka. Hiki ni kiwango kikubwa.”