Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Athari za IDAI za anika mzigo wa madeni ya siri Msumbiji-UN

Esther akiwa amesimama nje yachandarua anakoishi kufuatia kufurushwa na athari za kimbunga Idai nchini Msumbiji.
UNICEF/DE WET
Esther akiwa amesimama nje yachandarua anakoishi kufuatia kufurushwa na athari za kimbunga Idai nchini Msumbiji.

Athari za IDAI za anika mzigo wa madeni ya siri Msumbiji-UN

Tabianchi na mazingira

Athari za kimbunga Idai kilichoikumba Msumbiji na kwingineko kimeanika hadharani mzigo wa madeni ya siri ambayo hayajalipwa nchini Msumbuji kwa mujibu wa mtalaam wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa.

Mtaalam huyo Juan Pablo Bohoslavsky amesema "Ufahamu wa haki za binadamu za kiuchumi, kijamii na kitamaduni nchini Msumbiji haupaswi kuathiriwa na ulipaji wa madeni ya nchi na hasa sehemu yake ya 'mikopo ya siri.' Haki za Binadamu na athari kubwa za kimbunga Idai ni muhimu zikapewa kipaumbele katika mjadala kuhusu madeni”

Ameongeza kuwa "Nina wasiwasi sana kuhusu athari za haki za binadamu kwa muda mfupi na  muda mrefu. Haki za kibinadamu lazima ziwe katikati ya jitihada za kukabiliana na athari za kimbunga.Janga halipaswi kuongeza mzigo wa madeni na madeni hayastahili kuwa kikwazo cha juhudi za kukabiliana na athari za kimbunga hicho.”

Mwaka 2013 na 2014 mikopo isiyojulikana ya Serikali iliyohakikishiwa, ilikuwa na thamani ya jumla ya dola bilioni 2, na ilichukuliwa na vyombo vinavyomilikiwa na Serikali nchini Msumbiji bila idhini ya  bunge na yanazidi kiwango cha juu kilichowekwa na serikali. Upelelezi na mashtaka ya mahakama yanaendelea, na mabadiliko ya mfumo wa madeni na kuyafuta vyote vinaangaziwa.

Mtaalam huyo amesema "Mwaka wa 2016, tume ya Bunge ya Uchunguzi ilihitimisha kuwa dhamana za madeni hayo zilikiuka katiba , kinyume cha sheria, zilikiuka sharia za bajeti. Na tume ya ukaguzi wa hesabu za serikali ulibaini kwamba mchakato wa kutoa dhamana haukukidhi masharti na kulikuwa na uwezekano mkubwa wa maslahi binafi.”

Kufuatia ufunuo huo wa mikopo wa mwaka 2016, Shirika la Fedha duniani (IMF) na wakopeshaji wengine walisitisha msaada wa fedha Msumbiji. Madeni ya umma yaliongezeka.Na hivi karibuni IMF ilisema Msumbiji unahitaji kufikia kiwango cha kufutiwa madeni.

Mtaalam huyo ameitaka Msumbiji na wakopeshaji wake ikiwemo IMF kutathimini athari za haki za binadamu katika mikakati ya madeni, uwezekano wa mipango ya kubadilishwa au kufutiwa madeni hayo na pia mapendekezo  ya mabadiliko ya kiuchumi . Pia amewahimiza kuzingatia “athari za madeni hayo kwa haki za binadamu na misingi ya uwazi, ushirika wa umma na uwajibikaji kabla ya kutoa mikopo, akisema wakopeshaji wana wajibu wa kuhakikisha maafisa wa serikali wanapewa ridhaa chini ya sheria za madeni za nchi kabla hawajasaini mikataba”

Pia ameichagiza serikali kuongeza juhudi na kuhakikisha kwamba uchunguzi huru unafanyika kwa madai ya ufisani Msumbiji. Na kusema “Kwa kifupi madeni ya siri hayapaswi na hayawezi kulipwa.”