Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WFP yakaribisha ufadhili kutoka kwa USAID kwa ajili ya CAR

Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani, WFP likigawa chakula katika maeneo yenye mizozo kama DRC na CAR. Sehemu ya misaada hutolewa na wadau kama USAID.
WFP/Jacques David
Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani, WFP likigawa chakula katika maeneo yenye mizozo kama DRC na CAR. Sehemu ya misaada hutolewa na wadau kama USAID.

WFP yakaribisha ufadhili kutoka kwa USAID kwa ajili ya CAR

Msaada wa Kibinadamu

Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani, WFP limekaribisha ufadhili wa dola milioni 6 kutoka kawa mfuko wa Marekani wa maendeleo ya kimataifa USAID ambao utahakikisha huduma ya misaada kupitia anga, UNHAS inaendelea kwa ajili ya kuwasilisha msaada nchini Jamhuri ya Afrika ya kati, CAR.

Kwa mujibu wa taarifa ya msemaji wa WFP, Herve Verhoosel mjini Geneva, Uswisi, hii leo CAR imeghubikwa na mzozo wa miaka mingi huku kukizuka mapigano mara kwa mara ambapo barabara hazipitiki na maeneo mengi ndani ya nchi huwa yanatengwa kutoka kwa mji mkuu, Bangui na kuiacha UNHAS kuwa kama njia pekee ya usafiri kufikia maeneo ambayo ni vigumu kuyafikia.

Huduma hiyo ya anga ambayo inawezesha watoa huduma kufikia maelfu ya watu CAR, ilikuwa katika hatari ya kufungwa kufuatia ukata wa fedha.

WFP imekaribisha ufadhili huo kwani fedha walizo nazo zinamalizika Aprili mwa huu wakati huu ambapo mahitaji ya kibinadamu yanaongezeka.

UNHAS imekuwa ikifanya kazi CAR tangu mwaka 2006 na ni mhudumu pekee wa usafiri wa anga kwa mashirikia yasiyo ya kiserikali, Umoja wa Mataifa, mashirika ya ufadhili na jumbe za kigeni.