Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kutokana na mkataba wa amani, angalau hali ya usalama imetengamaa-Wakimbizi Sudan Kusini

Kituo cha Umoja wa Mataifa cha kulinda Raia, Wau, Sudan Kusini.
UN
Kituo cha Umoja wa Mataifa cha kulinda Raia, Wau, Sudan Kusini.

Kutokana na mkataba wa amani, angalau hali ya usalama imetengamaa-Wakimbizi Sudan Kusini

Amani na Usalama

Baada ya kuyakimbia mapigano katika Kijiji chao cha Ngovu na wakajificha karibu na kituo cha ulinzi wa raia cha Umoja wa Mataifa huko Wau, Sudan Kusini, Regina na Mayige Lina James sasa wamereja katika Kijiji chao wakiwa na matumaini kuwa makubaliano ya amani yatawaruhusu kuanza maisha yao upya. 

Kijiji cha Ngovu lilikuwa eneo la kuishi kwa  amani hadi mgogoro ulipoibuka kwenye eneo la Bahr El Ghazal Sudan Kusini mnamo mwezi Juni mwaka 2016 na kuwalazimisha maelfu ya familia kukimbia.

Regina Peter msichana mwenye umri wa miaka 19 alikuwa miongoni mwa wakimbizi wa ndani baada ya baba yake kuuawa katika kiji cha Ngovu. Alikimbilia karibu na Baggari nako akakuta hali mbaya.

(Sauti ya Regina Peter)

“Tulipofika kijiji cha Baggari tuliishi kichakani ambako mara kwa mara maji ya mvua  yalikuwa yanatuzoa. Na kulikuwa na mlipuko wa magonjwa mengi kama vile Malaria, kuhara na kutapika. Tulilazimika kutumia miti shamba kwa sababu hakukuwa na huduma za matibabu”

Familia ya Regina iliishia kuomba hifadhi katika kituo cha usalama wa raia cha Umoja wa Mataifa kilichoko umbali wa kilomita 15 kutoka Wau. Baada ya hali kuanza kutengamaa, Regina ameamua kuondoka kambini na kurejea katika Kijiji chao cha Ngovu. 

Kama ilivyo kwa Regina, mgogoro pia umemuathiri Mayige Lina James mwenye umri wa miaka 40. Alimpoteza mume wake, jambo ambalo limemfanya kushindwa kuwatunza Watoto wake watatu.

(Sauti ya Mayige Lina James)

“Kutokana na mkataba wa awali wa amani, hali ya usalama angalau imetengamaa kuliko ilivyokuwa awali. Kwa hivyo tunaomba kwamba mkataba ulosainiwa hivi karibuni kuwa halisi ili watu waweze kuishi pamoja bila migogoro. Suala ambalo bado linasumbua hivi sasa ni jinsi ya kupata kipato kwa ajili ya maisha bora”

Takribani wasudani kusini milioni 4.5 waligeuka kuwa wakimbizi tangu tangu mapigano yalipoanza katika mji mkuu Juba mwezi Septemba mwaka 2013. Watu milioni 2 kati yao wamekuwa wakimbizi wa ndani, na watu wengine milioni 2.5 wamesaka hifadhi katika nchi za jirani.