Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wakimbizi wanaovuka mpakani mwa DRC na Sudan Kusini waleta hofu ya Ebola:UNMISS 

Safari za mpakani kutoka Sudan Kusini hadi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC zinazua hofu ya uwezekano wa Ebola kusambaa.
UN Photo/Beatrice Mategwa
Safari za mpakani kutoka Sudan Kusini hadi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC zinazua hofu ya uwezekano wa Ebola kusambaa.

Wakimbizi wanaovuka mpakani mwa DRC na Sudan Kusini waleta hofu ya Ebola:UNMISS 

Wahamiaji na Wakimbizi

Safari za mpakani zinazofanywa na jamii za wakimbizi wa ndani kutoka Jjimbo la Yei nchini Sudan Kusini zimeanza kuzusha hofu ya uwezekano wa mlipuko wa Ebola kuingizwa ndani ya nchi hiyo kutokea nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC

Mpakani mwa Sudan Kusini na DRC, askari wa mpango wa Umoja wa Mataifa Sudan Kusini , UNMISS wakijipanga kwenda kushika doria kwenye mji wa Lasu jimboni Yei ambako wahudumu wa misaada wa mashirikaya Umoja wa Mataifa pia wako kusaidia maelfu ya wakimbizi wa ndani.

Hata hivyo UNMISS inasema wakimbizi kutoka Sudan Kusini ambao hivi sasa wanaishi kwenye kambi nchini DRC, baadhi yao mara nyingi huvuka mpaka kurudi nyumbani kusaka chakula kwenye nyumba zao walizozikimbia jimboni Yei kutokana na machafuko, hali ambayo inazusha hofu ya kuingiza Ebola ikizingatiwa kwamba DRC bado inakabiliana na ugonjwa huo.

Licha ya ulinzi kuimarishwa bado hatari ipo Luteni Kanali mstaafu Mwarambao Muralonya kutoka mkakati wa ufuatiliaji wa masuala ya ulinzi na usitishaji mapigano Sudan Kusini anafafanua kwa nini wanafanya hivyo

(SAUTI MWARAMBAO)

“Wanakuja upande huu kukusanya chakula tu kwenye mashamba yao ambayo yako upande huu wa Sudan Kusini, kwa sababu wakiwa huko nje hawapatiwi msaada wowote kama wakimbizi hivyo ni lazima waje hapa wapate chakula na kisha kurejea. Lakini hawakai hapa kwa sababu hali si nzuri hapa.”

Mmoja wa wakimbizi hao Jacob Karan akiwa kwenye bodaboda yake anathibitisha hilo

(SAUTI YA JACOB KARABA)

“Tangu tulipoondoka 2016 tulikuwa tunaishi vizuri kambini na tulikuwa tunapokea mgao wa chakula. lakini tangu mwanzoni mwa mwaka huu hatujapokea mgao wowote ndio maana tunakuja hapa Sudan Kusini kupata chakula.”

Mbali ya chakula pia wanafuata mahitaji mengine kama anavyosema mama huyu mkimbizi

(SAUTI YA MAMA MKIMBIZI)

“Nina mtoto mmoja, tulikimbia kutoka hapa nikiwa mjamzito, tulipita msituni na sasa tunaishi kwenye kambi ya wakimbizi DRC. Japo tunasikia kwamba hali imetengamaa vijijini kwetu bado hatujarejea. Kila wakati tunakuja hapa kukusanya nyasi kwa ajili ya kujengea nyumba zetu na kuuza baadhi ili kununua sabuni za kufulia. 

Na kwa upande wa DRC askari wa serikali walioko mpakani wanajitahidi kuwasaidia wakimbizi hawa ambao wanasema

(SAUTI ASKARI WA DRC)

Hivi sasa UNMISS ikishirikiana na serikali ya Sudan Kusini na wadau wengine wa afya wanachukua kila tahadhari kuhakikisha wanazuia mlipuko wa Ebola kuingia nchini humo.