Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Licha ya kupungua tatizo la ajira , uduni wa ajira hizo ndio mtihani-ILO Ripoti

Watoto na watu wazima kutoka Romania wakifanyakazi katika eneo la kutupa taka jirani na makazi ya Nadezhda nchini Bulgaria. Familia hizi zinakosa fursa za ajira, ambayo ndio kauli mbiu ya ripoti ya mwaka huu ya ILO kuhusu mtazamo wa ajira na mwenendo Duni
UNICEF
Watoto na watu wazima kutoka Romania wakifanyakazi katika eneo la kutupa taka jirani na makazi ya Nadezhda nchini Bulgaria. Familia hizi zinakosa fursa za ajira, ambayo ndio kauli mbiu ya ripoti ya mwaka huu ya ILO kuhusu mtazamo wa ajira na mwenendo Duni

Licha ya kupungua tatizo la ajira , uduni wa ajira hizo ndio mtihani-ILO Ripoti

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Ajira za viwango duni ni moja ya changamoto kubwa katika soko la ajira huku mamilioni ya watu wakilazimika kukubali mazingira duni ya kazi, kwa mujibu wa ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kazi duniani, ILO iliyotolewa leo.

Ripoti hiyo iliobeba jina: Ajira duniani na mwelekeo wa kijamii:mienendo 2019 inaonyesha kuwa idadi kubwa ya watu bilioni 3.3 walioajiriwa kote ulimwenguni mwaka 2018 hawana usalama wa kiuchumi, mali na usawa wa fursa. Isitoshe juhudi za kupunguza ukosefu wa ajira kimataifa hazionekani katika juhudi za kuimarisha viwango vya kazi.

Ripoti hiyo ya ILO imetoa mfano wa pengo katika ajira zenye hadhi huku ikionya kuwa katika viwango vya hatua za sasa, kufikia lengo la kazi yenye hadhi kwa wote kama ilivyopendekezwa kwenye malengo ya maendeleo endelevu hususan lengo namba 8 ni ndoto katika nchi nyingi.

Akizungumzia ripoti hiyo, Deborah Greenfield, naibu mkurugenzi mkuu wa sera wa ILO amesema, SDG 8 sio tu inalenga ajira, lakini viwango vya ajira yenyewe.” Akiongeza kuwa, “usawa na kazi bora ni vitu viwili tofauti kwa ajili ya maendeleo endelevu.

 

Upatikanaji wa chakula nao ni mgumu mjini aza kutokana na umaskini, usalama mdogo na ukosefu wa ajira.
WFP/Wissam Nassar
Upatikanaji wa chakula nao ni mgumu mjini aza kutokana na umaskini, usalama mdogo na ukosefu wa ajira.

Ripoti hiyo imetoa angalizo kuwa miundo ya biashara za kisasa ikiwemo zinazoendeshwa na teknolojia mpya, zinatishia kuathiri mafanikio yaliyopatikana kwenye soko la ajira katika maeneo tofauti ikiwemo katika kuimarisha ajira kuwa rasmi, usalama, ulinzi wa kijamii na viwango yya kazi isipokuwa watunga sera wakabiliane na changamoto hizo

ILO imesema ajira haimaanishi mtu atakuwa na maisha bora kwani watu milioni 7000 wanaishi na umaskini wa viwango vya wastani licha ya kuwa na ajira. Ripoti imetanabaisha kuwa ni hatua ndogo tu zimepigwa katika kuziba pengo la kijinsia katika kushiriki ajira ambapo asilimia 48 tu ya wanawake ndio wako katika soko la ajira ikilinganishwa na asilimia 75 ya wanaume. Aidha wanawake wanajumuisha idadi kubwa ya nguvu kazi walio na uwezo, ambao nguvu kazi yao haitumiwi ipasavyo.

Halikadhalika ripoti imeonyesha ongezeko la ajira zisizo rasmi huku watu bilioni 2 au asilimia 61 ya watu wakiwa katika kundi hilo. ILO inasema cha kusikitisha ni kuwa mtu mmoja kati ya watano walio chini ya umri wa miaka 25 hawana ajira, hawajasomo au kupokea mafunzo na hivyo kuhatarisha mustakabali wao wa ajira.

Ripoti hiyo ya kila mwaka imeonyesha hatua zimepigwa katika baadhi ya maeneo ambapo iwapo uchumi wa dunia hautadoroda, ukosefu wa ajira utapungua katika nchi nyingi. Vilevile kumekuwa na upungufu wa watu maskini wanaofanya kazi katika kipindi cha miaka 30 iliyopita katika nchi za kipato cha wastanni na ongezeko la watu wanaopata elimu na mafunzo.

'Bodaboda' za magurudumu matatu mjini Delhi India.Ripoti mpya ya ILO yasema  ajira milioni 24 kubuniwa ifikapo 2030
ILO/Vijay Kutty
'Bodaboda' za magurudumu matatu mjini Delhi India.Ripoti mpya ya ILO yasema ajira milioni 24 kubuniwa ifikapo 2030

Mtazamo kikanda

Ripoti inasema katika bara la Afrika asilimia 4.5 ya watu walio na umri wa kuajirawa hawana kazi huku asilimia 60 wameajiriwa. Hatahivyo, wafanyakazi wengi wanalazimika kufanya kazi duni ambapo nguvu kazi inatarajiwa kuongezeka kwa watu milioni 14 kwa mwaka na ukuaji wa kiuchumi unatarajiwa kuwa mdogo sana kubuni ajira zenye viwango.

Kwa upande wa nchi ya  Marekani ukosefu wa ajira unakadiriwa kupungua hadi asilimia 4.1 mwaka 2019  huku ukuaji wa ajira na uchumi vikitarajiwa kupunuga mwaka 2020. Amerika kusini na Caribea, ajira inakadiriwa kuongezeka kwa asilimia 1.4 tu mwaka 2019 na 2020 licha ya kushuhudiwa ukuaji wa uchumi.

 Katika mataifa ya Uarabuni ukosefu wa ajira unakadiriwa kusalia katika asilimia 7.3 hadi mwaka 2020 huku ukiongezeka katika nchi zisizoshirikiana na Gulf. Aidha wafanyakazi wahamiaji wanajumuisha asilimia 41 ya ajira kwenye kanda.

Nako Asia na pasifiki ukuaji wa kiuchumi unaendelea na ukosefu wa ajira unakadairiwa kusalia katika asilimia 3.6 kufikia 2020 chini ya viwango vya ulimwengu.