Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wamiliki wa radio wasiwabinye wanahabari ili sote tunufaike na matangazo ya radio- Msikilizaji

Radio ni mkombozi kwa watu wengi kwa kuwa  huwezesha kupata habari kwa kina kama hapa inavyoonekana kwa wakazi wa Sangari Jamhuri ya Afrika ya kati wakisikiliza Radio Lego Tila Ouaka( Sauti ya Ouaka) radio ya jamii inawaleta pamoja waislamu na wakristo
Picha ya OCHA/Gemma Cortes
Radio ni mkombozi kwa watu wengi kwa kuwa huwezesha kupata habari kwa kina kama hapa inavyoonekana kwa wakazi wa Sangari Jamhuri ya Afrika ya kati wakisikiliza Radio Lego Tila Ouaka( Sauti ya Ouaka) radio ya jamii inawaleta pamoja waislamu na wakristo

Wamiliki wa radio wasiwabinye wanahabari ili sote tunufaike na matangazo ya radio- Msikilizaji

Utamaduni na Elimu

Ikiwa leo ni siku ya radio duniani , kauli mbiu ikiwa majadiliano, uvumilivu na amani, mkoani Kagera nchini Tanzania wananchi nao wamepaza sauti kuhusu umuhimu wa njia hiyo adhimu ya mawasiliano na kile ambacho kinapaswa kufanyika ili kuhakikisha taarifa kutoka chombo hicho zina mantiki.

Miongoni mwa wananchi hao ni George Miyango mkazi wa Buyekera mjini Bukoba ambaye katika mazungumzo na Nicolas Ngaiza wa Radio washirika Kasibante FM anaanza kwa kuelezea  ufahamu wake kuhusu radio.

“Mimi ninavyofahamu redio ni kitovu cha mawasiliano makubwa na kuweza kupeleka habari kwa muda mfupi tofauti na ule upelekaji wa habari uliokuwepo, taarifa moja inaweza kuwafikia watu maelfu na maelfu kwa muda mfupi kuliko iliyokuwa inapeleka habari kwa farasi, kwa magari au kwa njia ya kupeleka vifurushi.”

Alipoulizwa kuwa radio inamsaidia vipi, Bwana Miyango amesema, “inanisaidia kupata habari za kijamii, kiuchumi na habari hata za vifo na vitu vingine ambavyo ninaweza kuwa sivielewi. Ninasikiliza redio hata nikiwa kwenye shughuli zangu na ninakuwa na redio.”

Hata hivyo amesema kuna changamoto kwenye kupata maudhui sahihi kwenye redio kwa sababu baadhi ya redio zina muegemeo mmoja au wa upande fulani kutokana na msimamo wa mmiliki wa radio.

Kwa mantiki hiyo amesema ni vyema wamiliki wa vyombo vya habari wasiegemee upande wowote na mamlaka zihakikishwe waandishi wa habari wako huru.

Amesihi watu wasio na  hulka ya kusikiliza redio wabadili mitazamo yao na kuanza kusikiliza redio kwa sababu “maarifa yanatafutwa, unaposoma ukisaidiana na magazeti na redio ndipo unakuwa kama unanoa maarifa  yako na unaweza kuwa mwanajamii bora na mwenye maarifa.”