Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto zaidi ya 3000 wameachiliwa na makundi yenye silaha Sudan Kusini:UNICEF

Waliokuwa askari watoto wakiwa wameachiliwa  Yambio Sudan, Kusini Febuary 2018
UNMISS/Isaac Billy
Waliokuwa askari watoto wakiwa wameachiliwa Yambio Sudan, Kusini Febuary 2018

Watoto zaidi ya 3000 wameachiliwa na makundi yenye silaha Sudan Kusini:UNICEF

Amani na Usalama

Maisha ya watoto wengine 119 yamenusurika leo baada ya kuachiliwa na makundi yenye silaha nchini Sudan Kusini na hivyo kufanya idadi ya watoto walioachiliwa tangu kuanza kwa mzozo nchini humo kufikia zaidi ya 3100.

Wasichana 48 ni miongoni mwa watoto walioachiliwa leo akiwemo mdogo kabisa wa miaka 10. Akizungumzia hatua hiyo mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF, Henrietta Fore amesema “Kila mtoto ambaye hayuko tena mikononi mwa makundi yenye silaha inamaanisha ni kurejesha utoto wake na mustakhbali wake”.

 Hata hivyo amesema “ingawa watoto wengi zaidi wanaachiliwa na makundi yenye silaha na vikosi vya serikali nchini Sudan kusini , na kwamba hili ni jambo linalotia moyo na matumaini , lakini bado safari ni ndefu kabla ya watoto wote 19,000 ambao bado wako jeshini kurejeshwa kwenye familia zao.”

Tangu mwezi Februari 2018 zaidi ya watoto 100 wameachiliwa huru na makundi mbalimbali yenye silaha. Tukio la leo limefanyika Kusini Magharibi mwa mji wa Yambio ambako Watoto awali walihusishwa na kundi la ukombozi wa taifa la Sudani Kusini (SSNLM) ambalo limetia saini mkataba wa amani na serikali mwaka 2016.

Wakati wa mchakato wa kuachiliwa huru Watoto wote walipewa vyeti vinavyoeleza kwamba wako huru na hawahusiani tena na kundi lolote lenye silaha na kisha wanakiutanishwa na wataalam wa ustawi wa jamii, wahudumu wa afya, na wataalm wa elimu ili kutathmini mahitaji yao , pia wanakabidhiwa nyenzo za kuwajumuisha tena katika jamii ikiwemo vifaa vya msingi kama nguo, viatu na vitu vingine.