Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dola milioni 43.5 zinahitajika mwaka huu kuimarisha huduma za afya Libya- WHO

Heleema mwenye umri wa miaka 42 akiwa amewabeba mapacha wake wenye umri wa miezi miwili kambini walikokimbilia baada ya mji wao wa Tawergha kilomita 600 magharibi mwa Benghazi Libya kushambuliwa.
UN OCHA/GILES CLARKE
Heleema mwenye umri wa miaka 42 akiwa amewabeba mapacha wake wenye umri wa miezi miwili kambini walikokimbilia baada ya mji wao wa Tawergha kilomita 600 magharibi mwa Benghazi Libya kushambuliwa.

Dola milioni 43.5 zinahitajika mwaka huu kuimarisha huduma za afya Libya- WHO

Afya

Shirika la afya duniani WHO na washirika wake wametangaza ombi la dola milioni 43.5 ili kuimarisha huduma za afya nchini Libya hususan kwa watu 388,000 walioathirika na mgogoro unaoendelea nchini humo.

Mwakilishi wa WHO nchini Libya Dkt Syed Jaffar Hussain, akizungumza hii leo mjini Cairo Misri amesema, “miaka mingi ya mgogoro nchini Libya imezorotesha mfumo wa afya ambao tayari ulikuwa umeelemewa. Vituo vingi vya afya vimefungwa kabisa au kwa kiasi fulani, hali inayozuia watu wengi ambao wameathirika na changamoto za miaka 8 ya mgogoro kuweza kupata huduma za kiafya.”

Taarifa iliyochapishwa katika mtandao wa WHO kanda ya Mediterania inasema tathimini iliyofanywa WHO pamoja na Wizara ya Afya mwaka 2017 kuhusu huduma ya afya na utayari, ilionesha kuwa asilimia 17.5 ya hospitali na asilimia 20 ya vituo vya afya na hospitali 18 za huduma maalumu zilikuwa zimesambaratishwa kabisa au kwa kiasi fulani na kwamba maeneo ya kutoa huduma za kiafya ambayo yanaendelea kutoa huduma yako katika hatari ya kushambuliwa, huku matukio 41 ya kuwalenga wahudumu wa afya yakiwa  yameripotiwa kwa mwaka 2018 hadi 2019 nchini humo.

Kukosekana kwa dawa muhimu na watoa huduma kunaongeza hatari ya kusambaa kwa magonjwa ya kuambukiza yakiwemo kuhara, kifua kikuu na magonjwa mengine amayo yangeweza kuzuilika kwa chanjo, taarifa ya WHO inasema.

Halikadhalika, wagonjwa wenye magonjwa ya kudumu na wenye uhitaji maalumu kama wagonjwa wa akili, wajawazito na watoto wachanga wako hatarini.