Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika ni mfano wa kuigwa katika suala la kuhudumia wakimbizi na wahamiaji.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akizungumza na vyombo vya habari mjini Addis Ababa Ethiopia 9 Februari 2019
screen grab/media stakeout video
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akizungumza na vyombo vya habari mjini Addis Ababa Ethiopia 9 Februari 2019

Afrika ni mfano wa kuigwa katika suala la kuhudumia wakimbizi na wahamiaji.

Wahamiaji na Wakimbizi

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres  hii leo baada ya mkutano wake na mwenyekiti wa Kamisheni ya Muungano wa Afrika, AU mjini Addis Ababa Ethiopia amewaeleza wanahabari kuwa  nchi za Afrika ni mfano kwa nchi tajiri wakati linapokuja suala la kuwahudumia wakimbizi.

Antonio Guterres yuko nchini Ethiopia kuhudhuria mkutano wa mwaka wa AU ambao huwaleta pamoja wakuu wa mataifa kutoka kote barani Afrika. Mkutano wa mwaka huu ambao unaanza jumapili hii utajikita katika masuala ya wakimbizi na wakimbizi wa ndani.

Bwana Guterres ambaye kabla hajachaguliwa kuwa mkuu wa Umoja wa Mataifa, kwa miaka 10 alikuwa mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi UNHCR, amesema katika bara la Afrika, mipaka iko wazi kwa wakimbizi na kuwa bara hili linaongoza pale linapokuja suala la kushughulikia wahamiaji.

UNHCR inasema kuwa nchi za kusini mwa jangwa la Sahara zinahifadhi zaidi ya asilimia 26 ya wakimbizi wote duniani.

Aidha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameeleza kuwa kinyume na mtazamo uliopo, ukweli ni kuwa wahamiaji wengi wa kiafrika wako katika nchi za Afrika kuliko Ulaya na uhamiaji barani Afrika umeshughulikiwa katika njia za kibinadamu zaidi. Guterres ametoa wito kuwa mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu wahamiaji na wakimbizi utekelezwe kikamilifu.