Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR yaomba radhi kwa Tanzania kutokana na sakata la nguo za msaada kwa wakimbizi zilizofanana na sare za kijeshi.

kamishina mkuu UNHCR Filipo Grandi
Arthur Max/FM. Ministério das Relações Exteriores
kamishina mkuu UNHCR Filipo Grandi

UNHCR yaomba radhi kwa Tanzania kutokana na sakata la nguo za msaada kwa wakimbizi zilizofanana na sare za kijeshi.

Wahamiaji na Wakimbizi

Kamishna Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR, Filipo Grandi akiwa ziarani nchini Tanzania  amesema Tanzania kwa muda mrefu imekuwa ni karimu hususan kwa wakimbizi ambao wanakimbia machafuko na rais wake John Magufuli amerejelea kuwa ukarimu huo hautafika mwisho.

 

Akizungumza na waaandishi wa habari pindi tu baada ya mazungumzo yao ya faragha na Rais John Pombe Magufuli, Ikulu jijini Dar es salaam, Bwana Grandi amesema,

“Tumejadili pia suluhu kwa sababu hatuwezi kubali suala la wakimbizi liwe la milele, kumekuwa na maendeleo nchini Burundi na baadhi ya watu wameelezea nia yao ya kurejea na rais ameafiki kuwa kurejea kwao lazima kuwe  kwa hiari na lazima iwe chaguo la wakimbizi na nipo hapa kufuatilia hilo kuhusu namna ya kusaidia wanaorejea kwa sababu tunahitaji fedha kwa ajili ya wanaorejea na kwa wale ambao hawako tayari kurudi makwao, tumejadili namna sio tu ya kuwasaidia wakimbizi lakini pia jamii zinazoathirika kutokana na uwepo wao ikwemo mazingira na usalama na kuimarisha ufadhili kwa sababu tunao mkataba kuhusu wakimbizi unaoturuhusu kufanya hivyo.” 

Kamishna huyo mkuu wa UNHCR aliulizwa swali kuhusu sakata la nguo zinazofanana na sare za kijeshi kubainika kuwa miongoni mwa nguo za msaada kwa wakimbizi wa Burundi mkoani Kigoma na hivyo amesema, “hili lilikuwa ni kosa, haukuwa mpango, ilikuwa ni sehemu ya shehena ya nguo kutoka kampuni kubwa nchini Japani. Na miongoni mwake kulikuwemo na nguo zinafanana na sare za kijeshi. Lilikuwa ni kosa ambalo hatukupaswa, hatujawahi kufanya lakini wakati mwingine vitu hivi hutokea. Nimemuomba radhi Rais na bila shaka hatutarudia tena.”

Arnold Kayanda/UNNewsKiswahili
Habari za UN

Kwa upande wake Rais Magufuli amezungumzia kile ambacho wamejadili akisema kuwa, "alichoeleza kikubwa ni kwamba ataendelea kutoa ushirikiano kwa nchi yetu ya Tanzania ambayo kwa miaka mingi imekuwa ni nyumba ya wakimbizi na hasa kulingana na hali halisi ya jografia ya nchi yetu na ameishukuru kwa kuendelea kusaidi wakimbizi na kwa upande wetu tumemueleza ukweli kwamba, Tanzania mpaka sasa inahifadhi zaidi ya wakimbizi 350,000, nimemuelezea kuwa Burundi hali inaendelea kuwa nzuri na kuna zaidi ya wakimbizi takriban 40,000 ambao wanategemewa kurudi kule na tunawashauri kwamba mambo si mabaya Burundi warudi makwao na amesema kwamba wataendelea kutoa msaada.”