Guterres atuma salamu za rambirambi Brazil baada ya bwawa kupasuka kuta na kuleta madhara
Kufuatia kupasuka kwa bwawa la maji huko Brumadinho jimbo la Minas Gerais nchini Brazil, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametuma salamu za rambirambi baada ya kuarifiwa kuwa baadhi ya watu wamefariki dunia na uharibifu wa mali na mazingira.
Vyombo vya habari vinaripoti kuwa hadi sasa miili 10 imepatikana na mamia ya watu hawajulikani walipo baada ya kuta za bwawa hilo kupasuka na kusababisha maji na matope kuenea kwenye makazi ya watu na mazingira.
Katibu Mkuu kupitia taarifa ya msemaji wake iliyotolewa leo jijini New York, Marekani ametuma salamu za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha na serikali ya Brazil, huku akiwatakia ahueni ya haraka majeruhi.
Amesema Umoja wa Mataifa uko tayari kusaidia mamlaka za Brazil kwenye harakati za uokozi kwenye janga hilo kusini mashariki mwa Brazil.