Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Daktari anayejitolea kuwasaidia manusura wa ISIL

Mwanamke wa kabila la Yazid akizungumza na Angelina Jolie, mjumbe maalum wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR.
UNHCR/A. McConnell
Mwanamke wa kabila la Yazid akizungumza na Angelina Jolie, mjumbe maalum wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR.

Daktari anayejitolea kuwasaidia manusura wa ISIL

Wanawake

Huko Kaskazini mwa Iraq, daktari wa kike kutoka jamii ya Yazidi anajitolea maisha yake kuwasaidia wanawake ambao walikuwa chini ya himaya ya kundi la ISIL lakini wakafanikiwa kutoroka.

Msimu wa kiangazi wa mwaka 2014 maelfu ya wanawake wa Yazidi na wasichana wanaoishi kaskazini mwa Iraq walitekwa na kufanywa watumwa na kundi la ISIL.  Wakiwa chini ya ISIL waliteswa na kunyanyaswa ikiwemo kubakwa. Wale ambao baadaye walitoroka au kuokolewa waliathirika kisaikolojia na pia maumivu ya mwili.

“Alituambia kuwa hatukuwa tu marafiki bali ndugu. Hilo lilitupa furaha. Alikuwa anatupa dawa na kutusaidia”

Sasa miaka miwili iliyopita Dkt Nagham Nawsat Hasan ambaye naye ni mkimbizi wa kabila la Yazidi, alianzisha shirika la kusaidia manusura wa ugaidi wa ISIL, na anawasaidia wanawake waliookolewa kutoka mikononi mwa kundi hilo kujenga maisha yao upya kwa kuwapatia ushauri wa bure na msaada wa kisaikolojia.

“Nimejitolea maisha yangu kuwahudumia wanawake wa Yazidi, manusura wa ISIL”

Daktari huyu bingwa wa magonjwa ya wanawake aliwahi pia kutoa msaada kwa myazidi Nadia Murat ambaye alishinda tuzo ya amani ya Nobel mwaka jana.

Hata wakati huu zaidi ya wanawake 1400 waliotekwa na kundi la ISIL nchini Iraq mustakabali wao haufahamiki.