Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuna walakin katika kutimiza Agenda 2030 kwa mwelekeo wa sasa-Bachelet

Watoto wakitembea katika jamii ya waRoma mji wa Shumen, Bulgaria Kaskazini.
© UNICEF/UNI154440/Pirozzi
Watoto wakitembea katika jamii ya waRoma mji wa Shumen, Bulgaria Kaskazini.

Kuna walakin katika kutimiza Agenda 2030 kwa mwelekeo wa sasa-Bachelet

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa, Michelle Bachelet amesema dunia haipo kwenye njia sahihi kufikia malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.

Amesema hayo akihutubia mkutano maalum wa Baraza la haki za binadamu mjini Geneva, Uswisi wa kuangalia hatua zilizopigwa katika kutimiza Agenda hiyo ya 2030.

Kamishna mkuu huyo amesema, “Ajenda ya 2030 ni dhamira ya kufikia ushirikiano mkubwa kimataifa kwa ajili ya usawa, lakini zaidi ya yote ni ahadi kwa watu ambao awali walitengwa kutoka kwa maendeleo: walisahaulika, wasio na nguvu na jamii ambazo hazishirikishwi; na mamilioni ya wanawake, watu wanaobaguliwa kwa rangi yao, dini au hadhi, jamii za watu wa asili, wahamiaji na watu walio na ulemavu na watu maskini.”

Bi Bachelet ametaja baadhi ya maeneo ambako kumepigwa hatua kubwa ikiwemo katika kukabiliana na umaskini, vifo vya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano, kuimarisha elimu hususan barani  Asia lakini akisema kuna vikwazo vingi ambavyo vinazuia maendeleo jumuishi kwa wote ikiwemo usawa wa kijinsia, njaa, vita na mabadiliko ya tabianchi.

Kamishna Mkuu huyo amesema, “mizozo inaharibu maisha ya watu, matumaini na uwezo wa watu kujipatia kipato ambapo watu 44,000 wanalazimika kukimbia makazi yao kila siku kwa ajili ya mizozo na unyanyapaa. Mabadiliko ya tabianchi yanaibua majanga ya kimazingira ambayo inaharibu miundombinu msingi na kuchochea uhasama na mizozo.”

Bi. Bachelet amehoji kama dunia inafikia lengo lake kuu la kuhakikisha kuwa haiachi mtu yeyote nyuma kufikia mwaka 2030 akinukuu takwimu za shirika la kazi ulimwenguni, ILO ambazo zinaonyesha kuwa pengo kati ya watu tajiri na maskini linaongezeka licha ya kuimariska kwa uzalishaji wa wafanyakazi.

Kwa mantiki hiyo amesema, “ikiwa imesalia miaka 12 tu kabla ya kufika 2030, tunahitaji hali mwamko wa haraka kuhusu kufikia ahadi hiyo kwa ulimwengu”.

Kwa upande wake rais wa mfuko wa Mary Robinson ambaye pia ni kamishna mkuu mstaafu wa haki za binadamu, Mary Robinson amesema, serikali katika maeneo mengi kote ulimwenguni zinashindwa kuwasilisha huduma muhimu ikiwemo huduma ya afya, elimu, makazi, huduma za kujisafi na maji safi bila uwajibikaji.  

Bi. Robinson amesihi chi na washika dau kuoanisha haki za binadamu na ajenda ya 2030 kwa kujumuisha ripoti za maendeleo na za haki za binadamu kwa kufanya kazi na washika dau na raasisi za haki za binadamu kwa ajili ya kuhakikisha uwazi na hatua sahihi.

 

TAGS: Michelle Bachelet, Mary Robinson, Agenda 2030, SDGs