Ongezeko la uhamiaji lasababisha watoto kuishia mitaani Djibouti- IOM
Hebu fikiria iwapo kazi yako ni kuombaomba mitaani, kusafisha magari, viatu na biashara ya ngono. Hebu fikiria iwapo njia moja ya kuimarsiha maisha yako inahitaji kuondoka nchi yako na kusafiri kilometa nyingi kufanya kazi katika mji mmoja wa Afrika na wakati huo ukiwa na umri wa miaka 11.
Hiyo ni hali halisi kwa watoto wapatao 1,137, kwa mujibu wa ripoti ya shirika la Umoja wa Mataifa la uhamiaji, IOM iliyotolewa leo ikilenga watoto nchini Djibouti ikipatiwa jina watoto waishio mitaani Djibouti.
Ripoti hiyo yenye lengo la kuonyesha hali ya maisha kwa watoto walioko mjini Djibouti inatokana na utafiti uliohusisha watoto 1,137 wenye umri wa kuanzia miaka 0 hadi 17 waliogundulika kuishi mitaani.
Kati yao hao, 633 wana umri wa kati ya miaka 0 hadi 9, ikiwemo wasichana 195 na watoto 504 walio na umri kuanzia miaka 10 hadi 17, ambapo 64 ni watoto wa kike.
Mtoto mmoja katika utafiti huo amesema kuwa anafanya kazi kwa saa nyingi kwenye mgahawa ambapo analipwa dola 56 kwa mwezi, fedha ambayo hata hivyo alituma nyumbani Ethiopia ili iweze kusaidia familia yake.
Mtazamo ni kwamba Djibouti huenda sio mahali ambapo watoto wataweza kuishi mitaani lakini hali ni hiyo ukizingatia kwamba ni kituo cha usafiri kwa wahamiaji wengi kutoka Ethiopia wanaolenga kuvuka mpaka kuelekea Yemen na nchi zingine za Kiarabu.