Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Biashara ya bidhaa za ubunifu imekua-UNCTAD.

Mkoba uliotengenezwa kutokana na ngozi ya Samaki
Video Capture/Unifeed
Mkoba uliotengenezwa kutokana na ngozi ya Samaki

Biashara ya bidhaa za ubunifu imekua-UNCTAD.

Ukuaji wa Kiuchumi

Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa imetoa ripoti yake inayoonyesha ongezeko maradufu la thamani ya biashara ya bidhaa zitokanazo na ubunifu kutoka dola bilioni 208 mwaka 2002 hadi dola bilioni 509 mwaka 2015.

Ripoti hiyo ambayo ni toleo la pili la tathmini ya uchumi utokanao na bidhaa za ubunifu imezinduliwa leo huko Geneva, Uswisi ambapo UNCTAD inasema kuwa China ndio inaongoza kwa kiasi kikubwa katika biashara hiyo ya bidhaa za ubunifu inayohusisha ubunifu wa majengo, mitindo ya mavazi na maonesho, usanifu wa ndani ya nyumba na hata sanaa za filamu na vikaragosi.

Akizungumza na wanahabari mjini Geneva wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo, Mkurugenzi wa kitengo cha biashara ya kimataifa na bidhaa UNCTAD, Pamela Coke-Hamilton amesema takwimu hizi ni muhimu kwa namna mbili, “uchumi wa kiubunifu una utajiri wa kibiashara na pia kiutamaduni. Thamani hizi mbili zinasababisha serikali duniani kote kujikita katika kukuza na kuendeleza uchumi wa kiubunifu kama kama sehemu ya mikakati ya mabadiliko ya kiuchumi na juhudi za kuhamasisha mafanikio na maisha bora.”

Aidha Bi Coke- Hamilton amesema tasnia ya ubunifu ambayo ni pamoja na usanifu majengo, sanaa na ufundi, masoko na matangazo ya biashara, vyombo vya habari na uchapishaji, utafiti na maendeleo, programu za kompyuta, michezo ya komputa na vingine vya namna hiyo ni msingi wa uchumi wa ubunifu.

“Katika uchumi wa ubunifu, tasnia ya ubunifu inazalisha kipato kupitia biashara na haki miliki pia inazalisha fursa mpya hususani kwa ajili ya makampuni madogo na yale ya kati” ameongeza Bi Coke- Hamilton.

China ni wasafirishaji wakubwa zaidi wa bidhaa na huduma za ubunifu. Katika mwaka 2002 biashara ya China katika bidhaa za ubunifu ilifikia bilioni 32 za marekani na kufikia mwaka wa 2014 kiwango hicho kimekua zaidi ya mara tano na kufikia bilioni 191.4 dola za marekani.