CENI yamtangaza Tshisekedi rais mteule DRC, Guterres atoa kauli
Tume ya huru ya taifa ya uchaguzi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, CENI imemtangaza Felix Antoine Tshisekedi Tshilombo kutoka chama cha UDPS, kuwa mshindi wa kiti cha urais kufuatia uchaguzi uliofanyika nchini humo tarehe 30 mwezi uliopita wa Desemba.
Ukurasa wa mtandao wa Twitter wa CENI umeonyesha kuwa Tshisekedi amepata asilimia 38.57 ya kura zote zilizopigwa akifuatiwa na Martin Fayulu Madidi wa muungano wa vyama vya upinzani aliyepata asilimia 34.83 ilhali Emmanuel Ramazani kutoka chama tawala akipata asilimia 23.84.
Les trois candidats en lice à l’élection présidentielle ont obtenu:1. Monsieur Félix Antoine TSHISEKEDI TSHILOMBO: 7.051.013 soit 38,57%. 2. Monsieur Martin FAYULU MADIDI: 6.366.732 soit 34,83%3. Monsieur Emmanuel SHADARY: 4.357.359 soit 23,84%Taux de participation: 47,56%
cenirdc
Kufuatia matokeo hayo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema anatambua taarifa hizo na amepongeza wananchi wa DRC na wanasiasa kwa vile waliendesha na kushiriki uchaguzi huo wa rais, majimbo na wabunge kwa kutoa fursa jumuishi ya ushiriki.
Kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake mjini New York, Marekani jumatano usiku, Bwana Guterres ametoa wito kwa wadau wote kujiepusha na ghasia zozote na kuwasilisha malalamiko yoyote ya mchakato huo kwenye mifumo iliyowekwa kwa mujibu wa katiba ya DRC na sheria nyingine husika za uchaguzi.
Katibu Mkuu ameelezea matumaini yake kuwa CENI, mahakama ya katiba, serikali, vyama vya siasa na mashirika ya kiraia watawajibika katika kuimarisha utulivu na kuheshimu maadili ya kidemokrasia ya taifa hilo.
Halikadhalika amesisitiza kuwa Umoja wa Mataifa utaendelea na ushirikiano na wadau wa kikanda na wale wa kimataifa katika kuimarisha amani, utulivu na maendeleo nchini DRC.
Hata hivyo wilaya tano nchini DRC hazikushiriki kwenye uchaguzi huu mkuu kutokana na sababu za kiusalama na ugonjwa wa ebola.
Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi iliyotolewa mwaka jana, Rais mteule anatarajiwa kuapishwa tarehe 18 mwezi huu wa Januari.