Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Matokeo ya uchaguzi DRC yakisubiriwa, hali ni tulivu ila tete- OHCHR

Upigaji kura wakati wa uchaguzi wa Rais na wabunge kwenye mji mkuu Kinshasa, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC tarehe 30 Desemba 2018
MONUSCO/John Bopengo
Upigaji kura wakati wa uchaguzi wa Rais na wabunge kwenye mji mkuu Kinshasa, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC tarehe 30 Desemba 2018

Matokeo ya uchaguzi DRC yakisubiriwa, hali ni tulivu ila tete- OHCHR

Haki za binadamu

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, OHCHR imesema hali nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC wakati huu ambapo matokeo ya  uchaguzi mkuu yanasubiri, ni tulivu ila tete.

Huku kukiwa na ripoti ya kwamba waandishi wa habari na wagombea kutoka vyama vyaupinzani wanakumbwa na vitisho na kuna vizuizi kuelekea katika baadhi ya vyombo vya habari, ofisi hiyo kupitia msemaji wake, Ravina Shamdasani imeonya kuwa hatua zozote za kuziba mdomo wapinzani zitakuwa na madhara.

Kauli ya Bi. Shamdasani imekuja saa chache kabla ya mashauriano ya faragha kuhusiana na uchaguzi huo kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani  baadaye leo.

Matokeo ya uchaguzi wa  rais uliofanyika tarehe 30 mwezi uliopita wa Desemba ukihusisha wagombea 21, yanatarajiwa kutangazwa jumapili hii ingawa tume ya uchaguzi DRC imesema kuwa inawezekana tarehe ikasogezwa mbele.

Wapiga kura wakiangalia majina yao kwenye orodha ya wapiga kura wakati wa uchaguzi wa rais na wabunge huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC tarehe 30 Desemba 2018
MONUSCO/Alain Likota
Wapiga kura wakiangalia majina yao kwenye orodha ya wapiga kura wakati wa uchaguzi wa rais na wabunge huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC tarehe 30 Desemba 2018

 “Kile ambacho wenzangu wamenijulisha na kwamba wameshuhudia ni kwamba ingawa hali ni tulivu bado ni tete kabla ya kutangazwa kwa matokeo hayo ya uchaguzi,” amesema msemaji huyo wa OHCHR akiongeza kuwa taarifa za awali zinaripoti matukio ya hapa na pale ya ghasia na baadhi ya watu wamejeruhiwa.

OHCHR imekuwa na ofisi yake kwenye taifa hilo la Maziwa Makuu Afrika lakini haijawa na dhima yoyote katika usimamizi wa uchaguzi huo ambao ulikuwa unaahirishwa tangu mwaka 2016.

Upigaji kura hata hivyo uliahirishwa hadi mwezi Machi mwaka huu katika wilaya tano kutokana na ukosefu wa usalama na mlipuko wa Ebola.

Sambamba na hayo, Bi. Shamdasani ameripoti uwepo wa ukiukwaji wa haki za raia ikiwemo kukatwa kwa huduma za intaneti akitolea mfano matangazo ya radio ya RFI ya Ufaransa pamoja na Televisheni ya Canal Congo inayomilikiwa na kiongozi wa upinzania Jean-Pierre Bemba nayo ilikumbwa na mushkeli.