Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtoto wa kwanza kwa mwaka 2019 azaliwa huko Fiji!

Mtoto mchanga wa kike ambaye amezaliwa ilipotimu saa sita kamili ya  tarehe mosi Januari 2019 huko Fiji.Mama y ake mzazi anaitwa Losena na ni miongoni mwa wajawazito wawili waliojifungua kati ya saa sita kamili na saa sita na dakika moja huko Fiji.
UNICEF/UN0269241/Chute
Mtoto mchanga wa kike ambaye amezaliwa ilipotimu saa sita kamili ya tarehe mosi Januari 2019 huko Fiji.Mama y ake mzazi anaitwa Losena na ni miongoni mwa wajawazito wawili waliojifungua kati ya saa sita kamili na saa sita na dakika moja huko Fiji.

Mtoto wa kwanza kwa mwaka 2019 azaliwa huko Fiji!

Afya

Heri ya mwaka mpya wa 2019 mfuatiliaji wa habari za Umoja wa Mataifa wakati huu ambapo chombo hicho kimeeleza kuwa takribani watoto 395, 072 watazaliwa siku hii ya kwanza yam waka.

Taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limesema kuwa asilimia 25 ya watoto hao watazaliwa barani Asia peke yake, likisema kuwa sambamba na kukaribisha mwaka mpya, wakazi wa dunia hii watasherehekea kuzaliwa pia kwa watoto.

Mtoto wa kwanza amezaliwa huko Fiji bahari ya Pasifiki ilhali mtoto wa mwisho kwa siku ya kwanza yam waka 2019 atazaliwa nchini Marekani.

Mchanganuo kwa ujumla unaonyesha kuwa India itakuwa na watoto wachanga 69,944, China 44,940, Nigeria 25,685, Pakistani 15,256, Marekani 11,086, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC 10,053 na Bangladesh 8,428.

Kwa kuzingatria kuwa mwaka 2017 watoto milioni 1 walifariki dunia mara tu baada ya kuzaliwa, UNICEF inataka hatua zaidi mwaka huu mpya kuepusha vifo vya watoto wachanga.

Mtoto mchanga akipokea chanjo ya polio katika hospitali mjini Abidjan, Ivory Coast.
UNICEF/Olivier Asselin
Mtoto mchanga akipokea chanjo ya polio katika hospitali mjini Abidjan, Ivory Coast.

“Hebu na tuazimie kukidhi haki ya kila mtoto kwa kuanzia na haki ya kuishi,” amesema Charlotte Petri, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF akiongeza kuwa, “tunaweza kuokoa mamilioni ya watoto iwapo tutawekeza kwenye mafunzo na vifaa kwa wahudumu wa afya mashinani ili watoto wachanga wazaliwe kwenye mikono salama.”

UNICEF imekumbusha kuwa mwaka 2019 ni miaka 30 tangu nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa zipitishe mkataba wa kimataifa wa haki za mtoto, CRC, tukio ambalo litasherehekewa duniani kote kwa matukio mbalimbali.

Kwa mujibu wa mkataba huo, nchi hizo ziliahidi kuchukua hatua ili kulinda kila mtoto kwa kumpatia huduma bora za afya, elimu, ulinzi na maendeleo.

Ingawa katika kipindi cha zaidi ya miongo mitatu, dunia imeshuhudia hatua bora za uhai wa mtoto, kwa kupungua kwa asilimia 50 idadi ya watoto wanaofariki dunia kabla ya kutimiza  umri wa miaka mitano, bado kuna maendeleo yasiyotia moyo katika kupunguza idadi ya watoto wanaofariki dunia chini ya umri wa mwaka mmoja.

Kwa mantiki hiyo UNICEF inatoa wito wa hatua za haraka za kuwekeza huduma ambazo kila mtu anaweza kumudu za kuhakikisha mtoto na mama yake wanapata huduma bora za afya.

Tafadhali iwapo unataka kupokea taarifa kutoka UN News Kiswahili kila wakati zinapochapishwa, tafadhali jisajili na pia unaweza kupakua apu ili kuweza kusikiliza wakati wowote popote ulipo.