Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waliokufa Indonesia kutokana na Tsunami sasa ni 281- OCHA

Mwezi Septemba Kisiwa cha Suwalesi nchini Indonesia kilikumbwa na tetemeko la ardhi na Tsunami. Zaidi ya watu 2,000 walifariki, 80,000 walipoteza makazi. Mtu huyu anatizama barabara na daraja lvilivyoharibika katika jiji la Palu
OCHA/Anthony Burke
Mwezi Septemba Kisiwa cha Suwalesi nchini Indonesia kilikumbwa na tetemeko la ardhi na Tsunami. Zaidi ya watu 2,000 walifariki, 80,000 walipoteza makazi. Mtu huyu anatizama barabara na daraja lvilivyoharibika katika jiji la Palu

Waliokufa Indonesia kutokana na Tsunami sasa ni 281- OCHA

Tabianchi na mazingira

Idadi ya watu waliofariki dunia kutokana na tsunami iliyokumba  maeneo ya mwambao mwa kisiwa cha Sumatra nchini Indonesia sasa imefikia 281 na wengine zaidi ya 1,000 wamejeruhiwa. 

Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na uratibu wa misaada ya dharura, OCHA  imesema pamoja na idadi hiyo ya vifo na majeruhi, hadi sasa watu 57 hawajulikani waliko huku wengine takribani 11,700 wamepoteza makazi yao.

Ikinukuu shirika  la kitaifa la Indonesia  linalishughulikia majanga-BNPB, OCHA imesema pamoja na madhara ya tsunami hiyo kwa binadamu, baadhi ya miundombinu na majengo vimeharibiwa, zikiwemo nyumba 611, hoteli 69, maduka 60 na mashua 420.

Tsunami hiyo ilipiga Indonesia Jumamosi na inasadikiwa chanzo ni maporomoko ya ardhi ndani bahari yaliyochochewa na mlipuko wa volkano ya Anak Krakatau katika eneo la mlango wa bahari wa Sunda.

Wimbi hilo kubwa la Tsunami liliathiri zaidi wilaya za Pandegland na Serang zilizoko katika mkoa wa Banten na pia wilaya zingine  mbili katika mkoa wa Lampung kwenye kisiwa cha Sumatra.

Vikosi vya usalama na mashirika mbalimbali ya ndani mwa nchi hiyo vinaendelea kutoa msaada.

Hadi sasa serikali haijaomba msaada ingawa  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, katika salamu zake za rambirambi kwa serikali ya Indonesia mwishoni mwa juma, amesema kuwa Umoja wa Mataifa uko tayari kutoa usaidizi iwapo utaombwa kufanya hivyo.

Tafadhali iwapo unataka kupokea taarifa kutoka UN News Kiswahili kila wakati zinapochapishwa, tafadhali jisajili na pia unaweza kupakua apu ili kuweza kusikiliza wakati wowote popote ulipo.