Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Zilizovuma mwaka 2018

Kutoka kushoto: Bendera ya UN ikipepea New York; Naibu Katibu Mkuu akiwa na nakala ya ripoti ya  UNCTAD; Walinda amani wa UN; Katibu Mkuu akiwa na wanawake viongozi waandamizi wa UN
UN
Kutoka kushoto: Bendera ya UN ikipepea New York; Naibu Katibu Mkuu akiwa na nakala ya ripoti ya UNCTAD; Walinda amani wa UN; Katibu Mkuu akiwa na wanawake viongozi waandamizi wa UN

Zilizovuma mwaka 2018

Masuala ya UM

Mwaka 2018 ulighubikwa na changamoto nyingi hususan kwa nchi za Afrika, mizozo ikiendelea kukumba bara hilo sambamba na magonjwa. Hata hivyo kulikuwa na habari chanya, na kwa muhtasari tutaangazia pande zote za sarafu wakati huu ambapo tunafunga mwaka huu wa 2018.
 

Tangu tarehe 1 Januari mwaka 2018, Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa imekuwa mstari wa mbele kukupasha siyo tu kile kinachoendelea kwenye makao makuu ya umoja huo jijini New York, Marekani bali pia ni kwa jinsi gani maamuzi yanayopitishwa na chombo hicho chenye wanachama 193 yanatekelezwa huko mashinani.

Na katika kukuletea taarifa hizo iwe kwa njia ya maandishi, sauti au video, Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa imezungumza si tu na viongozi wa umoja huo bali pia wananchi huko mashinani ambao ndio waathirika wa maamuzi hayo.

Katika toleo hili la matukio ya mwaka basi, tunakuletea habari ambazo zilisomwa zaidi, au zilikuwa na mashiko zaidi kuanzia masuala ya maendeleo, amani, usalama na kibinadamu. Mathalani Ebola ilivyotikisa tena Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, lakini mikakati ya serikali ilisaidia udhibiti wa mapema. Mchakato wa amani Sudan Kusini na makubaliano mapya yanayoleta nuru bila kusahau mabadiliko ya tabianchi, changamoto za ulinzi wa amani DRC na Rebeca Gyumi ambaye ni mmoja wa washindi wanne wa tuzo ya haki za binadamu ya mwaka 2018.

Na kwa habari zaidi za mwaka mzima unaweza kubofya hapa.

Kwa mshirika wetu, msomaji na shabiki wetu, Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa inakushukuru kwa kuwa nasi mwaka 2018 na inakutakia heri na ustawi kwa mwaka mpya wa 2019.

HABARI

1. Ebola yaibuka tena DRC

Chanjo za Ebola zikiandaliwa tayari kupatiwa wakazi wa Mbandaka huko jimboni Equateur nchini DRC.
WHO/Oka
Chanjo za Ebola zikiandaliwa tayari kupatiwa wakazi wa Mbandaka huko jimboni Equateur nchini DRC.

8 Mei 2018 - Ebola yabisha tena hodi DRC, ikiwa ni takribani mwaka mmoja tangu mlipuko mwingine utokee nchini humo kipindi kama hiki na kudhibitiwa baada ya miezi mitatu.

Serikali ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC hii leo imetangaza mlipuko wa Ebola huko Bikoro jimbo la Equateur.  Tangazo hilo linafuatia maabara ya kitaifa ya kitabibu huko Kinshasa, kuthibitisha visa viwili kati ya sampuli tano zilizowasilishwa kwa uchunguzi. Soma zaidi hapa

Tafadhali iwapo unataka kupokea taarifa kutoka UN News Kiswahili kila wakati zinapochapishwa, tafadhali jisajili na pia unaweza kupakua apu ili kuweza kusikiliza wakati wowote popote ulipo.

SAUTI

1. Kuhudumia watu wangu ndio wito wangu:Dkt. Atar

 

Dkt. Atar Adaha akiwa na mkimbizi kutoka Sudan ambaye nasubiri kufanyiwa upasuaji kwa ajili ya kujifungua kwenye Hospitali ya Maban, Kaunti ya Bunj, Sudan Kusini.
UNHCR/Will Swanson
Dkt. Atar Adaha akiwa na mkimbizi kutoka Sudan ambaye nasubiri kufanyiwa upasuaji kwa ajili ya kujifungua kwenye Hospitali ya Maban, Kaunti ya Bunj, Sudan Kusini.

01 Oktoba  2018 - Unapokuwa daktari wito wako ni kufanya kila liwezekanalo ili kuokoa maisha ya watu wanaokuhitaji, iwe katika mazingira mazuri au katika mazingira magumu, na kwangu hilo ndilo la muhimu. Amesema hayo Dkt. Atar Adaha, mshindi wa tuzo ya wakimbizi ya Nansen 2018, kutokana na kazi kubwa anayoifanya kama daktari bingwa wa upasuaji nchini Sudan Kusini. Sikiliza kwa kina.

VIDEO

1. Buriani

23 Novemba 2018 - Nchini Tanzania hii leo walinda amani watatu wa taifa hilo waliouawa katika matukio tofauti ya mapigano huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR wameagwa rasmi katika tukio lililoongozwa na Waziri wa Ulinzi Dkt. Hussein Mwinyi.