Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Somalia yatangaza vita dhidi ya ufisadi

Picha za shughuli mbalimbali nchini Somalia.
UN Photo/Ilyas Ahmed)
Picha za shughuli mbalimbali nchini Somalia.

Somalia yatangaza vita dhidi ya ufisadi

Sheria na Kuzuia Uhalifu

Serikali ya Somalia imetangaza  mikakati ya kuimarisha vita dhidi ya ufisadi na kuimarisha uwazi ili kujenga  taasisi ambazo zinawajibika.

Waziri wa Sheria na masuala ya kisheria  wa Somalia , Hassasn Hussein Haji  ametangaza hayo mjini Mogadishu wakati wa sherehe za kuadhimisha siku ya kupinga ufisadi, sherehe ambayo iliungwa mkono na Umoja wa Mataifa.

Waziri  alitangaza azma ya serikali yake  ya kukuza uwajibikaji na pia kufutualia ufisadi katika ngazi zote za serikali huku akitia saini kile kilichoitwa mpango wa kuanzisha mradi-PIP kati ya wizara yake na shirika  la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP, wenye lengo la kuimarisha taasisi za serikali ili kupigana dhidi ya ufisadi na pia  kukuza uwajibikaji.

Waziri Hussein amesema, “ tuko mbioni kuunda tume ya kupinga ufisadi, na inahitaji ofisi, na wanahitaji mafunzo katika maeneo yote.Kwa hivyo nadhani mradi huu utatuongoza  kukuza taasisi hii ambayo itatuwezesha  kutia saini na kuridhia  mkataba wa Umoja wa Mataifa dhidi ya ufisadi.”

 Akizungumza kwa niaba ya Umoja wa Mataifa, Naibu Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Peter de Clercq, ameipongeza serikali ya Somalia  kwa juhudi zake kuboresha  uwazi, uwajibikaji na vita dhidi ya ufisadi katika ofisi za umma, na pia kuihimiza kuendeleza juhudi za kuelekeza kufuata mkataba wa Umoja wa Mataifa dhidi ya ufisadi, chombo  alichoita, ndiyo “pekee duniani halali kinachohusika na vita dhidi ya ufisadi ambao hadi sasa mataifa 186 yameshauridhia.”

Baada ya sherehe ya kutia saini, mkuu wa UNDP nchini Somalia, George Conway, akaeleza  kuwa mradi huo mpya unairuhusu serikali ya  Somalia kukabiliana kikamilifu na ufisadi.