George Herbert Walker Bush aliuunga mkono Umoja wa Mataifa kwa moyo wake wote.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres kupitia taarifa iliyotolewa leo jumamosi, ameeleza masikitiko yake kutokana na kifo cha aliyekuwa rais wa 41 wa Marekani George H.W. Bush aliyefariki dunia jana Ijumaa.
Guterres amesema kuwa rais Bush ambaye aliiongoza Marekani mwaka 1989 hadi 1993 akiwa ametanguliwa na Ronald Reagan na kisha baada yake akafuatia Bill Clinton, alikuwa kiongozi wa tofauti na aliiuunga mkono Umoja wa Mataifa kwa moyo wote.
Rais Bush alikuwa na historia ndefu na Umoja wa Mataifa: kati ya mwaka 1971 na 1973 alikuwa mwakilishi wa kudumu wa Marekani katika Umoja wa Mataifa na mwaka 2005 aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati huo, Kofi Annan, alimteua kuwa mwakilishi wake maalum katika janga la tetemeko la ardhi katika Asia ya kusini.
Bwana Guterres amesema, “George H. W. Bush alifanya kazi nzuri na za tija katika Umoja wa Mataifa. Kwa miaka mingi niliendelea kuvutiwa na huruma yake, na kujitolea kwake katika huduma za kijamii. Katika kipindi hiki cha majonzi, ninatuma salamu zangu za rambirambi kwa familia yake, marafiki na serikali, pia kwa watu wa Marekani”