Ushirika wa mataifa ya kusini ni ufunguo wa maendeleo - Balozi Mero
Mkutano wa ushirikiano baina ya nchi zinazoendelea au nchi za kusini ukiendelea katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa, jijini New York, Marekani, Tanzania imesema kuwa ushirikiano huo umekuwa na manufaa sana hasa misaada ya maendeleo isiyo na masharti ya kupindukia licha ya kupigwa vita na baadhi ya watu.
Mkutano huo wa siku tatu unaleta pamoja wawakilishi wa nchi hizo zinazoendelea na taasisi ambazo zinasaidia kupigia chepuo ushirikiano huo yakiwemo mashirika ya Umoja wa Mataifa.
Miongoni mwa washiriki ni mwakilishi wa kudumu wa Tanzania kwenye Umoja wa Matifa Balozi Modest Mero ambaye amesema wamenufaika katika ushirikiano wa teknolojia, kilimo, uvuvi na zaidi ya yote ,« Na sasa hivi kumekuwa na kuanzisha benki ya nchi za kusini ambayo itakuwa inatoa mikopo nafuu ili kuharakisha maendeleo ya nchi za kusini, ili waweze kushiriki katika biashara ya kimataifa na uchumi wa kimataifa. Nikamuuliza Balozi Mero madai ya kwamba baadhi ya ushirikiano baina ya nchi za kusini ni mtego kwa nchi maskini, ambapo amesema.
« Hiyo ni propaganda tu. Na ni propaganda ya waliotutawala. Propaganda hiyo inajaribu kuepusha kwamba zile nchi zilikuwa makoloni yao haziwezi kuwa na mshirika mwingine kasoro wao tu ili waendelee kuwanyonya. Lakini ukweli ni kwamba mashirikiano za nchi za kusini ambazo zimepiga hatua, kama vile India, China, Indonesia, Brazil, Argentina ni mashirikiano ambayo yana uwiano sawa. Ni mashirikiaono ambapo mnakaa mezani mnakubaliana hatua za kuchukua ili kuongeza maendeleo. Ikiwa mnataka kupeana tekenolojia basi mnapeana kwa masharti nafuu. Fedha za mitaji , mnapeana kwa masharti nafuu, lakini pia kunakuwa na mpango maalum wa kuweza kutoa misaada ambayo hata wengine inakuwa ni bure sababu tu ni kuwa uwezo wa nchi kama China au India ni mkubwa na mara nyingi hutoa misaada ya bure ambayo inaitwa grants.”