Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF yaingiwa hofu juu ya hali ya watoto wahamiaji mpakani mwa Mexico na Marekani

Kundi la wasichana kutoka katika msafara wa wa wakimbizi kutoka nchi za Amerika ya Kati wakiwa katika kiwanja cha mpira cha Jesús Martínez 'Palillo kilicho kusini mwa mji mkuu wa Mexico, Mexico city
UNIC Mexico/Antonio Nieto
Kundi la wasichana kutoka katika msafara wa wa wakimbizi kutoka nchi za Amerika ya Kati wakiwa katika kiwanja cha mpira cha Jesús Martínez 'Palillo kilicho kusini mwa mji mkuu wa Mexico, Mexico city

UNICEF yaingiwa hofu juu ya hali ya watoto wahamiaji mpakani mwa Mexico na Marekani

Haki za binadamu

UNICEF ina wasiwasi mkubwa juu ya usalama na ustawi wa zaidi ya watoto wahamiaji 1,000 walioko kwenye msafara huko Mexico au wakisubiri huko eneo la mpakani la Tijuana wakati huu ambapo madai yao ya kusaka hifadhi yakishughulikiwa na mamlaka za Marekani.

Hivyo ndivyo ilivyoanza taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iliyotolewa  hii leo mjini New York, Marekani ikisema kuwa watoto hao wana fursa finyu ya kupata huduma za msingi ikiwemo lishe, elimu, matibabu na zile za kisaikolojia.

Taarifa hiyo imesema watoto hao wako hatarini pia kukumbwa na ukatili, uteswaji na hata kusafirishwa kiharamu wakati wakiwa kwenye msafara huo barabarani au wakiwa kwenye kambi za hifadhi zilizojaa pomoni.

“Mazingira hayo magumu wanakumbana nayo baada ya kukimbia ghasia, mateso,  umaskini uliokithiri huko walikotoka kwenye nchi zao za kaskazini mwa Amerika ya Kati,” imesema taarifa hiyo.

Wafanyakazi wa UNHCR wakisaidia watu katika mpaka wa Mexico na Guatemala ambao wamewasili na msafara wa wakimbizi na wahamiaji kutoka Honduras Oktoba 21, 2018
© UNHCR/Julio López
Wafanyakazi wa UNHCR wakisaidia watu katika mpaka wa Mexico na Guatemala ambao wamewasili na msafara wa wakimbizi na wahamiaji kutoka Honduras Oktoba 21, 2018

“Kwanza mtoto ni mtoto, bila kujali hali yake ya uhamiaji. Kwa mujibu wa sheria za kimataifa, UNICEF inasihi serikali zote kuwapa hakikisho la hifadhi watoto wote waliofurushwa kutokana na madhila na wapatiwe hifadhi bila kuchelewa bila kujali wameingia vipi kwenye nchi husika,” imesema taarifa hiyo.

Halikadhalika taarifa imesema UNICEF inasihi serikali kwenye ukanda huo wa Amerika ya Kati kuhakikisha familia zinakuwepo pamoja na kutumia maeneo mbadala badala ya kuwasweka ndani katika vituo vya kuhifadhi wahamiaji.

“Vituo vya kusubiria vya uhamiaji na kusweka ndani wanafamilia ni kitendo kinachosababisha kiwewe na kinaweza kuacha watoto wakiwa katika mazingira hatarishi ya kutumikishwa au kuteswa,” imesema ripoti hiyo.

Pamoja na hiyo wametaka serikali zirejelee hatua za kuhakikisha zinashughulikia chanzo cha uhamiaji usiofuata kanuni, sababu ambazo ni pamoja na umaskini, ghasia na ukosefu wa fursa za kiuchumi na elimu na kwamba UNICEF iko tayari kushirikiana na serikali kwenye ukanda huo kuhakikisha watoto hao waliokimbia makwao wanapatiwa  huduma na usaidizi unaohitajika.