Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kesi ya mbabe wa kivita Ntabo Ntaberi Cheka imeanza kuunguruma DRC:

Walinda amani wa MONUSCO kutoka Afrika Kusini wakiwa na raia wakati wa doria huko Kivu Kaskazini
MONUSCO
Walinda amani wa MONUSCO kutoka Afrika Kusini wakiwa na raia wakati wa doria huko Kivu Kaskazini

Kesi ya mbabe wa kivita Ntabo Ntaberi Cheka imeanza kuunguruma DRC:

Sheria na Kuzuia Uhalifu

Kesi ya mbabe wa zamani wa kivita kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC Ntabo Ntaberi Cheka imeanza kusikilizwa mjini Goma jimbo la Kivu ya Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo.

Kesi hiyo iliyoanza kuunguruma tarehe 24 Novemba mwaka huu inaendeshwa na mahakama ya kijeshi. Cheka alikuwa akiongoza kikosi cha ulinzi dhidi ya Congo almaarufu kama Ndumba defense of Congo au NDC, ambacho ni moja ya vikundi vyenye silaha vilivyoshambulia vijiji kwenye jimbo la Kivu ya Kaskazini nchini DRC kwenye eneo la Walikale.

Cheka alisalimu amri kwa walindaamani wa Umoja wa Mataifa (MONUSCO) tarehe 26 Julai 2017. Na MONUSCO walimkabidhi Cheka kwa mamlaka ya DRC kwa ajili ya kufunguliwa kesi. Gavana wa Goma Julien Paluku  akizungumzia kuhusu kuanza kwa kesi hiyo amesema, " Leo  sisi tuna furaha kwa sababu watu wote waliopatwa na shida na hata kupoteza ndugu zao (waliofariki), leo  watajikuta na  furaha kumwona yule ambaye walikuwa wanamuwazia kuwa ni mtu mkubwa ambaye hawezi kuguswa sasa yuko mahakamani. Na hiyo ni kitu kikubwa sana  na mimi nawaza itasaidia wale wote wanaojitokeza kufanya vitendo vya ugaidi wataona kuwa siku moja watakuwa mbele ya sheria."