Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nyumbani ni mahali hatari zaidi kwa uhai wa wanawake:UNODC

Mjini Mexico City sanaa zikiwakilisha wanawake , kwa kusisitiza ukubwa wa janga la mauaji ya kijinsia (femicidal) March 2018
UN women/ Dzilam Mendez
Mjini Mexico City sanaa zikiwakilisha wanawake , kwa kusisitiza ukubwa wa janga la mauaji ya kijinsia (femicidal) March 2018

Nyumbani ni mahali hatari zaidi kwa uhai wa wanawake:UNODC

Wanawake

Ripoti mpya iliyotolewa leo na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya madawa na uhalifu , UNODC inasema nyumbani ni mahali hatari zaidi kwa wanawke na hususan kwa mauaji na ukatili wengi wakipoteza maisha mikononi mwa wenzi wao au familia.

Ripoti hiyo inasema wanawake 87,000 waliuawa mwaka jana , huku 50,000 au asilimia 58 ikiwa ni mikoni mwa wenzi wao au jamaa watu wa familia. Hii inamaanisha wanawake 6 huuawa kila saa moja na watu wanaowafahamu umesema utafiti wa ripoti hiyo.

Matokeo ya utafiti huo yaliyotolewa kwa ajili ya kuadhimisha siku ya kimataifa ya kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake, yameangalia takwimu zizlizopo za mauaji na kutathimini mauaji yanayohusiana na masuala ya jinsia kwa wanawake na wasichana yakijikita zaidi kwa mauaji kutoka kwa wapenzi na watu wa familia na jinsi gani yanahusiana na hali na jukumu la mwanamke katika jamii kwa ujumla.

Akifafanua kuhusu ripoti hiyo mkurugenzi mtendaji wa UNODC,  Yury Fedotov amesema “Wakati wengi wa waathirika wa mauaji ni wanaume, wanawake wanaendelea kulipa gharama kubwa kutokana na kutokuwepo usawa wa kijinsia, ubaguzi na tabia mbaya. Pia wana uwezekano mkubwa wa kuuawa na wapenzi wao  na ndugu wa karibu katika familia, "

Ameongeza kuwa ili kukabiliana na uhalifu huo "Hatua madhubuti za haki dhidi ya uwahalifu zinahitajika ili kuzuia na kumaliza mauaji yanayohusiana na jinsia. UNODC imetoa ripoti ya utafiti huu kwa ajili ya siku ya kimataifa ya kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake 2018 ili kuongeza uelewa na kuwajulisha kuhusu hatua. "

Utafoiti huo uumebaini kwamba kiwango cha kimataifa cha mauaji ya wanawake na wasichana yanayofanywa na wenzi wao au wanafamilia ni mwathirika 1.3 kwa kila wanawake 100,000.

Katika kuangalia wapi kulikoathirika Zaidi utafiti umegundua kwamba Afrika na ukanda wa Amerika ndiko wanawake waliko hatarini Zaidi kuuawa na wenzi wao au wanafamilia. Na kwa Afrika kiwango ni wanawake 3.1 kwa kila wanawake 100,000, wakati nchi za Amerika ni wanawake 1.6 , Ocenia 1.3 na asia 0.9. Eneo lililo na kiwango kidogo kabisa kwa mujibu utafiti huo ni Ulaya ambako kiwango ni 0.7 kwa kila wanawake 100,000.

Ripoti hiyo imehitimisha kwa wito wa kuhimiza hatua za kuzuia uhalifu na na zadhani kwa ukatili dhidi ya wanawake ambazo zitachagiza usalama wa waathirika na kuwawezesha , lakini wakati huohuo kuhakikisha uwajibukaji wa hali ya juu kwa watekelezaji wa uhalifu huo.

Pia imetaka kuwe na uratibu mzuri na ushirikiano miongoni mwa polisi na mifumo ya haki na sheria, mifumo ya afya, na huduma za jamii ,na pia kuwahusisha wanaume katika kupata suluhu ya jinamizi hili ikiwemo katika elimu ya mapema.