Mashambulizi hayakatishi azma yetu ya kupambana na Ebola DRC:WHO
Shirika la afya duniani WHO limesema kazi za kupambana na mlipuko wa ugonjwa Ebola Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo DRC baado zinaendelea licha mashambulio yaliyofanywa Ijumaa katika mji Beni nchini humo.
Taarifa iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi, na shirika hilo inasema ingawa wafanyakazi wa WHO, wafanyakazi wa wizara ya afya ya DRC na wa washirikia wengine wako salama, lakini ilibidi wafanyakazi 16 wa WHO kuhamishiwa Goma kwa matibabu ya kisaikolojia baada ya makazi yao kushambuliwa na kombora ambalo halikulipuka.
Hata hivyo WHO imesema kazi za kupambana na Ebola ziliendelea mwishoni mwa juma mjini Beni ingawa kwa kiwango kidogo. Taarifa hiyo imefafanua kuwa zoezi la kutoa chanjo lilisimamishwa na vituo kadhaa kufungwa, lakini timu chache zilibaki zikikutana na wananchi hususan kwenda katika maeneo ambako iliripotiwa kuwa huenda kuna visa vya Ebola, na pia kuwajulia hali wagonjwa na vilevile kuwapeleka wagonjwa wengi katika vituo vya matibabu. Na vituo vinavyoendeswa na washiriaka wao viliendelea kufanya kazi kama kawaida.
Mkurugenzi mkuu wa WHO, Dkt Tedros Aghanom Ghebresyesus, amesema kuwa shirika lake litaendelea kufanya kazi bega kwa bega na wizara ya afya ya DRC na washirika wake kuweza kukabiliana na mlipuko wa Ebola nchini humo . Ameongeza kuwa wanakumbukwa wale wote waliopoteza maisha yao katika mlipuko huu na kulaani vikali vitisho vya kiusalamadhidi ya wale waliojitoa kuendelea kupambana na ugonjwa huo nchini DRC.