Kulikoni watu kulazimishwa kwenda uhamishoni?
Ibara ya 9 ya tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa linalotimiza miaka 70 mwaka huu wa 2018, inaeleza kuwa hakuna mtu anayepaswa kukamatwa kiholela na kuwekwa ndani au kulazimishwa kwenda uhamishoni. Lakini je! Nchi wanachama zinatimiza matakwa ya ibara hii?
Katika mazungumzo na Arnold Kayanda, Mwanasheria, wakili Jebra Kambole wa Tanzania anasema nchi nyingi zimejaribu kuwa na katiba na sheria zenye vifungu vinavyoendana na Ibara hiyo ya 9 ya tamko la haki za binadau.
Hata hivyo amesema mara kwa mara serikali zimekuwa zikitunga sheria mpya ambazo zinaenda kinyume na Ibara hii jambo ambalo linadhohofisha juhudi za Umoja wa Mataifa katika kuwafanya wanadamu waoishi kwa amani katika maeneo yao.
Amesema , “unakuta watu wanakamatwa na kuwekwa ndani kwa muda mrefu pasipo kufunguliwa mashitaka, na wakati mwingine watu wananyimwa dhamana katika mazingira ambayo walistahili kupewa dhamana.
Kuna haja ya Umoja wa Mataifa kushinikiza serikali zinazokiuka ili zianze kufuata msingi wa Ibara hii” anashauri wakili Jebra.