Huduma za afya kwa wote zijumuishe wagonjwa wa kisukari- WHO
Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya ugonjwa wa kisukari, shirika la afya ulimwenguni WHO linaangazia athari za kisukari kwa familia na majukumu ya wanafamilia katika kusaidia kinga, uchunguzi na usimamizi unaotakiwa kwa ugonjwa huo ambao ulisababisha vifo vya watu milioni 1.6 mwaka 2016.
Huyu ni Lucy John Bosco kutoka Tanzania mmoja wa zaidi ya watu milioni 400 wanaoishi na ugonjwa wa kisukuri hivi sasa duniani, hapa akielezea dalili za ugonjwa huo.
Katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, Lucy ambaye ugonjwa wa kisukari umekuwa sehemu ya maisha yake kwa miaka 17 sasa anaona kama ni mwenye bahati.
Lucy ambaye sasa ni mhamasishaji aliyesomea kozi maalum ya dalili za ugonjwa huo, anasema mafunzo yamekuwa ni kinga kubwa kwake kwa kuwa… kuna changamoto nyingi.
Kwa mujibu wa WHO, ugonjwa wa kisukari ni moja ya sababu kuu za watu kufariki mapema, upofu, figo kushindwa kufanya kazi, kiharusi na mtu kukatwa mguu na licha ya hayo, huleta mzigo mkubwa wa kiuchumi katika familia kutokana na gharama kubwa za kuhudumia mgonjwa.
Ni kwa mantiki hiyo WHO inatumia siku ya leo kuchagiza huduma za afya kwa wote inayohusisha pia matibabu ya wagonjwa wa kisukari.